domingo, 13 de março de 2016

MTU ANATHAMINI ZAIDI KULIKO MAKOSA YAKE


Kutafakari kutoka Yoh 8, 1-11

       Andiko hili linatuletea tukio la mwanamke ambaye alifumaniwa katika uzinzi na kutusaidia kutafakari kuhusu jambo muhimu katika sheria ya wayahudi na maisha ya binadamu, yaani, hali ya umoja kati ya mume na mke kupitia ndoa. Umoja huu ulichukuliwa kama mtakatifu na kubarikiwa na Mungu tangu mwanzo. Katika mpango wake wanapaswa “kuwa mwili mmoja”. Lengo la umoja huu ni kwa kuzaa watoto na kupata utimilifu kwa wanandoa. Mungu alijua kwamba umoja huu ulihitaji kulindwa na, kwa hivyo, alianzisha kama amri “Usizini na Usitamani mwanamke asiye na wako”. Alisema hivyo kwa sababu yeye ni wa kwanza anayejua kwamba bila umoja binadamu haishi vyema na bila uaminifu umoja hauwezekani.
    Wale ambao walimleta mwanamke huyo mbele ya Yesu walitenda dhambi ya udhalimu mara mbili. Ya kwanza ni kwa sababu uzinzi unawezekana tu kati ya watu wawili. Ikiwa washitaki hao walimleta mwanamke peke yake kumshitaki na kumwachia huru mwanamme, walitenda dhidi ya sheria wenyewe. Kulingana na kitabu cha Walawi (Wal 20, 10), “kama mwanamume akizini na mke wa jirani yake, ni lazima wote wawili wauawe.” Ya pili ni kwa sababu hao washitaki walijua kwamba wao wenyewe hawakuwa wasafi. Walikuwa wasio na haki na hata walitaka kwamba Yesu atende kulingana na matendo yao. Ishara zilizofanywa na Yesu zilikuwa nafasi ya watafakari kwamba maisha ya mtu ni bora kuliko sheria; ya kutafakari pia kuhusu umuhimu wa mwanamke katika jamii; tena kuhusu haja ya uhusiano wa kweli na Mungu pia na wengine, na kumpea mtu nafasi moja zaidi kama vile Mungu anavyofanya kwa ajili ya wenye dhambi, kwa sababu hataki kifu cha mwenye dhambi bali atubu na kupata uzima. Katika mwendo huu, Yesu aliamsha dhamiri zao kuhusu udhalimu wa ubaguzi akiwafanya kufikiri na kutenda tofauti. Kupitia njia ya Yesu ya kutenda, moyoni mwao waliweza kukiri kwamba wao pia walikuwa wadhambi na hivyo walihitaji msamaha wa Mungu. Kama matokeo, wote walisamehewa na Yesu, yaani, washitaki na mshitakiwa kwa sababu Yesu anataka kujenga jamii mpya kupitia uhusiano mpya kati ya watu.
       Kuhusu mwanamke huyo, alibaki katika mahali kamili, yaani, katikati; lakini sio kama rejeo ya hukumu bali kama rejeo ya huruma. Yeyote anayekutana na Kristo anakutana na huruma ya Mungu na kupata nafasi ya kuishi maisha mapya. Mwanamke yule alikuwa amekufa na amefufuka, alikuwa amepotea na ameonekana. “Enenda zako; wala usitende dhambi tena”. Yesu hakuja kuadhibu bali kuokoa; kwa hivyo maneno na ishara zake zinamsaidia mwanamke achukue ahadi ya kuishi tofauti, kulingana na mapenzi ya Mungu. Maneno haya yanaonyesha kwamba Yesu hakubali udhalimu wala hapitishi kosa lolote. Anatarajia mabadiliko ya maisha. Kwake mtu anathamini zaidi kuliko makosa yake. Kuhusu hili, yako maneno ya Mt. Yohana Calabria yanayosema, “tunapaswa kuyachukia makosa ya mtu, lakini tunapaswa kumpenda mtu huyu kwa sababu ndiye ndugu yetu”. Upendo unatufanya kusadiki kwamba inawezekana kubadilisha hali mbaya kuwa hali nzuri. Tunapompenda mtu tunausadiki uwezo wake wa kushinda udhaifu na mwelekeo mbaya wa maisha yake. Kwa upande wa mtu aliyependwa hii ni nafasi ya kuonyesha kwamba anaweza kujibadilisha.

    Maneno ya Yesu yalikuwa faraja na kusababisha kitendo tofauti. Ishara zake zilikuwa makaribisho na kusababisha mabadiliko ya maisha. Ikiwa maneno na ishara zetu zinatokana na msukumo wa Mungu zinapaswa kusababisha matokeo kama hayo. Mwanamke huyo ni mfano wa watu ambao wanahukumiwa na kuadhibiwa miongoni mwetu. Mawe ni alama ya maneno na ishara ambazo hazijatumika kwa kujenga ndugu, zikitia moyo na kuimarisha imani yao, bali zimewazuia kuamini kwamba wanaweza kubadilisha maisha yao na kufikia matarajio ya Mungu. Sisi pia ni kama mwanamke huyo. Baada ya kila mkutano na Bwana, hasa kupitia sakramenti, tunaalikwa kuiacha dhambi na kuchukua mwelekeo mpya wa kuishi. Neema ya Mungu ituongoze.

Fr Ndega 
Mapitio na marekebisho: Sara

Nenhum comentário: