domingo, 27 de março de 2016

MASHAHIDI WA BWANA MFUFUKA


Kutafakari kuhusu Matendo 10: 34a. 37-43; Yoh 20,1-9

Tufurahi sote, kwa sababu hii ni siku Mungu aliyotufanyia! Tangazo la ufufuko wa Yesu ni mwaliko wa furaha, yaani furaha ya maisha ambayo yanayashinda mauti, furaha ya upendo ambao unaushinda uchungu na kutenda kama rafiki katika safari ya watu wapya wa Mungu, kuyaimarisha matumaini yao. Wanafunzi wa kwanza walipotangaza tukio hilo, walianza kutokana na maisha ya binadamu ya Yesu, aliyetiwa na Mungu kwa kazi ya wokovu wa binadamu. Kwao Wanafunzi wa kwanza uzoefu pamoja na Yesu ulikuwa umejaa maana. Kutokana na uzoefu huu wanaweza kutenda kama mashahidi. Kama alama ya wema wa Mungu, maana ya maisha ya Yesu ilikuwa kuwatendea watu mema. Nalo tendo lake liliwezekana kwa sababu Mungu alikuwa pamoja naye. Alitaka kuupendekeza uzoefu wa maana kabisa kwa wale ambao watakuwa mashahidi wake.
Kama Kristu hakuwa amefufuka, je, mahubiri ya wanafunzi wake yangekuwa na maana gani? Hakika yangekuwa tupu, yaani, pasipo maana. Mbele ya kifo kisicho na haki cha mwalimu wao walikufa moyo sana, lakini ushindi wa uhai unawapa maana mpya ya kuishi. Basi, ujumbe wa wanafunzi unatafsiri pia ushindi dhidi ya hali ya hofu ambayo waliishi baada ya kifo cha Mwalimu, yaani kikundi chao kilivunjika. Kwa wanafunzi ilikuwa vigumu sana kuendelea kwa safari baada ya kukatishwa tamaa kwao kuhusu  mwalimu Yesu ambaye walitarajia mengi, hasa awe mfalme mwenye nguvu. Lakini maisha yao yalibadilishwa kabisa baada ya kuona ushahidi wazi wa ufufuko wa Mwalimu, yaani kaburi tupu, vitambaa alivyolalia, na baadaye Yeye mwenyewe akajionyesha kwao; kisha waliacha hofu, wakiitoa nafasi kwa imani na kuchukua maisha ya mashahidi. Ni njia kamili ambayo tunapaswa kuishi ili tuwe wanafunzi wa Yesu wa kweli.     
Lakini tunapaswa kutambua kwamba safari hii ya imani ya wanamume ilisababishwa na mwanamke, yaani Maria Magdalena ambaye alikuwa na upendeleo wa kuwa ni wa kwanza kuenda kaburini, kukutana na Yesu na kupewa habari kwa ajili ya Mitume. Walipaswa kuiacha picha ya Yesu kama alivyokuwa alipoteseka, amekufa na kuzika ili wakaribishe njia mpya ya Yesu aliye mzima na anayeishi kati yao kwa njia mpya na tofauti kabisa. “Magdalena ni yule ambaye Yesu aliponya kwa kufukuza mashetani saba ndani yake. Katika Biblia namba saba inamaanisha ukamilifu. Basi, Maria Magdalena alikuwa ameponywa na Yesu kikamilifu.” Katika Kristo Maria alikuta upendo wa kweli ambao alikuwa ameutafuta sana kwa muda mrefu. Mwanamke huyo alijifunza jinsi ya kuwa mwanafunzi wa kweli, akimfuata Yesu wakati wa mahubiri, tangu Galilaya hadi msalabani. Kwa hivyo anastahili cheo cha “Mtume wa Mitume wa Yesu.” 

Baada ya kupokea habari kuhusu udidimizi wa mwili wa Kristo, wanafunzi wawili wakaenda mbio kuelekea kwenye kaburi, yaani Petro na mwanafunzi aliyependwa na Yesu (Yohane). Walikimbia pamoja, lakini huyo mwanafunzi alifika kwanza. Kama hivi ni upendo ambao unapaswa kufika kwanza katika kila kitu. Yule anayependa anapata kuwa wa kwanza katika maonyesho ya upendo na imani. Anaweza kutambua mabadiliko kandokando yake, kwa sababu yeye mwenyewe ana moyo ambao umebadilishwa na uzoefu wa kujiona kupendwa. Uzoefu wa ufufuko ni uzoefu wa upendo wa Mungu anayetuchagua tumtumikie na kutubadilisha kabisa ili tuwe mashahidi wa upendo unaozaa uzima, unatufanya kushinda vikwazo, hofu na mashaka na kutufanya kuishi kwa hamu uzoefu wa ndugu. Kuhusu Petro, ndiye alama ya mapigano daima ya mtu ili aweze kushinda kuchoka kwa kazi; ni alama pia ya mtu ambaye anajaribiwa kufa moyo, lakini anashinda kwa sababu ya uzoefu mkubwa wa kujitolea ulio muhimu kwa kuwaongoza na kuwashauri wengine. Ushuhuda wetu kama mashahidi wa Bwana Mfufuka uwe kama ilivyotokea na wao. Tumsifu Bwana Mfufuka!  

Fr Ndega
Mapitio na marekebisho: Sarah

Nenhum comentário: