sábado, 4 de junho de 2016

MUNGU AMEWAANGALIA WATU WAKE


Kutafakari kuhusu 1Waf 17, 17-24; Wag 1, 11-19; Lk 7, 11-17

Liturujia ya jumapili hii inatualika kuona huruma ya Mungu kwa kwa ajili ya wote wanaoteseka. Mungu anaguswa na hali yetu na kutenda kwa huruma kwa sababu hii ndiyo tabia yake mwenyewe na kwa sababu tena anataka tujifunze kutoka kwake mfano mzuri wa kutenda. Turuhusu kusaidiwa na neno lake ambalo linaimarisha imani yetu na kuutoa mwelekeo kamili kwa maisha yetu. Neno hili ni kweli kinywani mwa Eliya alipompa mama mjane mtoto wake aliyefufuka. Hili tena ni kweli kupitia mahubiri ya Mtakatifu Paulo alipoutangaza ufunuo wa Yesu Kristo kama habari iliyojaa maana. Neno hili linaendelea kusababisha hali mpya kabisa maishani mwa wote ambao wanamtumainia Mungu.
Katika sehemu ya mwisho injili inaongea kwamba “habari hii ikaenea katika Uyahudi wote. Na katika nchi zote za kando kando. Hii ni habari kuhusu kutembelea kwake Mungu kuwakomboa watu wake kupitia Yesu aliye Nabii mkuu. katika Yesu Mungu anajifunua kama aliye karibu sana na mwenye unyeti sana. Kwa hivyo ni halali kusema kwamba Mungu wetu anao “moyo”. Tulisherehekea hali hii katika Ijumaa iliyopita kupitia Sherehe ya Moyo Mtakatifu wa Yesu. Yesu mwenyewe alisema kwamba Yeye yu mpole na mnyenyekevu wa moyo. Katika moyo wake zinakaa hazina za hekima na elimu. Kutokana na moyo wake tumeona tendo la huruma ya Mungu. Mfano wake wa unyeti ni mwaliko wa kuboresha tabia za wema na upole kama alama ya utunzaji wa Mungu. Habari ya njia maalum ya Mungu ya kuwajali watu wake inapaswa kutangazika. Habari hii inaiimarisha imani na kuyafufua matumaini kama ilivyotokea maishani mwa mama yule mjane ambaye alikuwa amempoteza mwanawe wa pekee, lakini akampokea tena kwa sababu ya hisia za moyo wa Yesu.
“Wakati Yesu alipomwona mama yule... akamwonea huruma.” Injili zote zinamjulisha Yesu kama yule aliyeguswa na mahangaiko na mateso ya watu. Huruma ni tabia yenyewe ya moyo wake. Huruma hii inamsukuma kutenda vitendo, ili kuwapunguzia wanaoteseka uzito wa mateso na mahangaiko yao. Mbele ya mahangaiko ya wanadamu Mungu amejibu daima kwa jibu kamili ambalo linaonyesha njia maalum yake ya kupenda. Upendo wake si kitu cha kinadharia bali “kwa mwonekano wake unaonyesha kitu cha kushikika: nia, mitazamo na tabia zinazoonyeshwa katika maisha ya kila siku.” Njia maalum ya Mungu ya kujibu mbele ya maumivu ya kibinadamu inamaanisha mahangaiko ya upendo wake kwetu. Watu walitambua huruma na ukombozi wa Mungu kupitia tendo la Yesu. Hivyo, walifikia lengo la utume wa Yesu, yaani, kudhihirisha huruma ya Mungu. “Kila kitu ndani yake kinaongelea huruma. Hakuna chochote kwake kinachopungukiwa na huruma. Tendo lake kwa ajili ya maisha ya watu linafunua kwamba Mungu anatamani wawe wenye afya njema; anataka kuwaona wenye furaha, wenye kujaa furaha na amani."

            Kanisa linatufundisha kutangaza kwamba “moyo wa Yesu ni chemchemi ya huruma” na Neno la Mungu lenyewe linashuhudia kwamba “Kwa upande wake tumepokea neema juu ya neema”.  Tunaalikuwa kuamini kwamba Yesu ni mwenye unyeti sana mbele ya hali yetu hasa nyakati za maumivu na huzuni, ambazo zinaonekana kwamba sisi tumeachwa peke yetu. Katika Kristo Mungu ni mwenye unyeti hasa kwa kutufundisha njia kamili ya kuwa binadamu wa kweli, yaani, njia ya kusaidiana na kumpa Mungu nafasi ya kutenda maishani mwetu kwa nguvu ya upendo wake. Yeye tunayemwamini ni Mungu wa uhai naye amependezwa kutushirikisha katika uzima wake wa milele, kwa sababu sisi tu wanawe wapendwa. Tujihakikishie kwamba Mungu hawezi kutuacha wala kunyamaza mbele ya kinachotokea kwetu. Ikiwa katika Yesu, yeye anajifunua kama ufufuko na uzima, tunapaswa kutangaza kwamba Mungu hataki kifo. Hali hii inatupa matarajio kuhusu kufufuka kwetu na maisha kamili kwani yeye si Mungu wa wafu bali wa wanaoishi. Kulingana na mapenzi yake maisha yetu yanafaa kupata ukamilifu. Neema ya Mungu iimarishe imani yetu katika riziki yake kwa sababu yeye yupo karibu nasi daima na hawaachi kamwe wale wanaomwamini.

Fr Josuel Ndega
Mapitio na marekebisho: Sarah

Nenhum comentário: