sexta-feira, 24 de junho de 2016

ALISAMEHEWA KWA SABABU ALIPENDA SANA

Kutafakari kuhusu Lk 7:36-8,3



     Tukio hili la mwanamke mwenye dhambi lilitokea humo nyumbani kwake Simoni Mfarisayo, aliyemwalika Yesu kula chakula. Yesu Alipokuwa mezani akila pamoja na wageni wengine mwanamke huyo anayefahamika kama mwenye dhambi akatokea na kuanza kumkaribia Yesu akimwonyesha ishara za upendo na shukrani kwa sababu aliuona msamaha na upendo wa Mungu katika hali yake ya dhambi. Ingawa Simoni alichukwa ahadi ya mwaliko, ni Yesu mwenyewe aliyetaka kukutana na Simoni na kumwongozea njia mpya ya kuishi. Kwa kweli Simoni alihitaji njia mpya, mtazamo mpya na kadhalika. Alimwalika Yesu lakini hakujua jinsi ya kumkaribisha vizuri. Yeye alisahau ishara za msingi kama zilivyokuwa desturi miongoni mwa Wayahudi, yaani, hakumpa Yesu maji kwa miguu yake; hakumbusu Yesu akionyesha kwamba alipendezwa na kutembelea kwake; hakumpaka kichwa chake Yesu mafuta.

      Katika injili ya Luka, Yesu anapenda kushiriki pamoja na watu katika chakula. Kwa kushiriki milo na watu wa aina na ngazi zote katika jamii, Yesu alionyesha kuwa yeye alikuwa wa watu wote, matajiri na maskini pamoja. Tukumbuke wakati alipokula chakula nyumbani kwake Mathayo pamoja na wenye dhambi wengi; tukumbuke pia wakati alipojikaribisha mwenyewe kwa karamu nyumbani mwa tajiri Zakayo. Kutembelea kwake Yesu kunasababisha mabadiliko maishani mwa watu kuwaongoza kufikiri na kutenda tofauti. Katika injili ya leo, ingawa alikuwa Simoni ambaye alimwalika Yesu nyumbani kwake, ni mwanamke fulani ambaye alimkaribisha vizuri. Mwanamke huyo ingawa hana jina, yaani heshima, hata hivyo ana ishara ambazo Yesu alitarajia kukuta kutoka kwa Simoni aliyejiona amejaa heshima. Mtazamo wa upungufu wa Simoni uliona kwanza udhaifu na makosa ya mwanamke. Lakini Yesu alimwalika Simoni kuona vizuri, akisema, “unamwona mwanamke huyo?” Huu ni mwaliko wa kuanza tena na kuona tofauti, kama Yesu mwenyewe alivyo. Yesu anajua dhambi nyingi za mwanamke huyo, hata hivyo anatambua kwanza ishara nyingi za upendo ambazo zinashinda udhaifu wake. Kwa upande wa Yesu upendo unashinda dhambi naye mtu anathamini zaidi kuliko makosa yake.  

         Katika mazingira yale, Simoni ni mmoja miongoni mwa waliojiona kuwa wenye haki na kwa hivyo, walijiona pia kwa mamlaka ya kuwachagua baadhi ya watu na kuwakataa wengine. Yesu anaukubali mwaliko wa Simoni, lakini haukubali mwelekeo wake wa kumhukumu mwanamke aliye miguuni mwake. Yesu anataka kwamba Simoni atambue kuwa mgawanyiko kati ya watu wazuri na wabaya haukubaliki mbele ya Mungu. Katika njia ya Mungu ya kutenda ubaguzi hauko. Pendo na huruma yake yapatikana kwa wote. Kwa hivyo Yesu alimsamehe mwanamke huyo na kupendekeza toba kwa wengine. Hili ni sharti ili huruma ya Mungu iwe ufanisi maishani mwao. Kama hivi Yesu alitangaza ufalme wa Mungu na wale ambao walimfuata waliruhusu kuguswa na huruma ya Mungu. Ni jambo la ajabu kwamba injili hii inaanza kwa mwanamke bila jina na kuhitimisha kwa majina kadhaa ya wanawake, yaani, Mariamu, Yohana, Susana na wengine wengi waliopokea tena heshima yao kwa sababu ya mkutano na Yesu na huruma ya Mungu.


      Kama ilivyotokea kwa mwanamke huyo, sisi pia tunaalikwa kujiona kukaribishwa na kubadilishwa kwa sababu ya mkutano na huruma ya Mungu hasa kupitia uzoefu wa sakramenti ya kitubio na upatanisho. Uzoefu huu tena unatusaidia kuushinda mwelekeo wetu wa kibinadamu wa kuwahukumu wengine na kuuona makosa yao kuliko tabia zao nzuri. Wakati tunapowahukumu tunajiona wenye haki, yaani tunajiona bora kuliko wengine. Je, ni nani aliye mwenye haki mbele ya Mungu? Tunaalikwa kuweka juhudi zaidi ili tuweze kuwaona wengine kwa mtazamo wa Yesu. Kama ilivyotokea katika tukio la mwanamke, Yesu anaona upendo wetu kwa kanisa, kwa jumuiya, kwa familia juu ya yote. Nao upendo wetu unaonyeshwa kupitia uzoefu wetu wa kusamehe, wa kuwakaribisha wengine vizuri na kuwatendea mema. Kusamehe ni asili ya Mungu (Kut 34:6). Hatuununui msamaha wa Mungu kwa mapendo yetu bali tunaupokea kwa hiari. Ekaristi hii takatifu itusaidie kupenda na kusamehe kama Mungu alivyo. 

Fr Josuel Ndega
Mapitio na marekebisho: Sarah

Nenhum comentário: