sábado, 4 de junho de 2016

MOYO SAFI KABISA WA BIKIRA MARIA


Kutafakari kutoka Is 61: 9-11; Lk 2: 41-51

Tunaadhimisha kumbukumbu ya moyo safi kabisa ya Bikira Maria. Kumbukumbu hii ni uenezi wa sikukuu ya Moyo Mtakatifu wa Bwana ambayo tulisherehekea jana. Tunaalikwa kutafakari kuhusu uwezo wa Mama Maria wa kuweka moyoni mwake Neno la Mungu na kuzaa tunda zuri kwa ajili ya dunia kulingana na mpango wa Mungu. Tunaalikwa kutafakari pia mshikamano wa Mariamu mbele ya mateso ya mwana wake kama ushirika wa mioyo miwili.

          Somo la kwanza, kutoka kitabu cha Isaya, linaongea kuhusu uhusiano wa kina kati ya Mungu na watu wake. Yeye anaitumia nguvu yake ili atende matendo ya ajabu kwa ajili ya wokovu wa watu wa Israeli. Mungu ni mwaminifu kwa watu hawa na kuahidi kuanzisha agano jipya la milele, kuuthibitisha ukaribu wake nao na kuwaalika kuishi uhusiano naye kwa hisia ya miliki. Uhusiano huu na Mungu unawahakikishia baraka nyingi na kuwabadilisha kuwa mfano kwa mataifa yote. Hali hii inafanana na ndoa, yaani, Mungu ni kama mume na watu kama mke. Watu wanaalikwa kwa shukrani na furaha kwa sababu Bwana mume wao ametenda makuu kwa ajili yao, akiwavalisha kwa wokovu na ushindi. Jumuiya ya kikristu hutafsiri hali ya mke huyo kama mfano wa Bikira Maria ambaye alikuwa mtumishi mwaminifu akikubali kumzaa Yesu kwa ajili ya wokovu wa ulimwengu mzima.

       Injili inaongea kuhusu ushiriki wa Familia takatifu (Yesu, Maria na Yosefu) katika jumuiya yake. Ushiriki wa Familia hii katika jumuiya ulikuwa desturi. Miongoni mwa Wayahudi kila Myahudi anapaswa kwenda Yerusalemu angalau mara moja kwa mwaka kwa sababu ya sherehe ya pasaka pamoja na wengine. Hivyo, Yesu alikuwa kijana wa umri wa miaka kumi na miwili, na ilionekana alipotea hekaluni, lakini kwa kweli yeye alijikuta mwenyewe kwa sababu kwa kuhusishwa na kushughulika kuhusu hali ya Baba yake kunampendeza. Hali hii ilikuwa ngumu sana kwa wazazi wake wafahamu. Lakini walikuwako tayari kuyakaribisha na kuyatenda mapenzi ya Mungu. Hasa kwa upande wa Bikira Maria, ingawa hakufahamu vizuri hali hiyo, alikuwa na tabia nzuri ya kuweka moyoni mwake mambo hayo yote, akitafakari na kutafsiri ili atende mapenzi ya Mungu. Kama hitimisho, mtoto Yesu alirudi Nazareti pamoja na wazazi wake na alikuwa anawatii. Hata utiifu kwa Mungu ulikuwa utambulisho wa wana wa familia hii. 

      Kulingana na kumbukumbu ya leo, tunaalikwa kuulenga uangalifu wetu kwenye moyo wa mama Bikira Maria, aliye mfano maalum wa mtumishi, wa mke na wa mwanafunzi kwa wote. Maria aliishi uhusiano wa ndani na Mungu kwa sababu moyo wake ulikuwa mali ya Mungu na ulikuwako kwa Mungu. Maria alikuwa makini sana kwa matendo ya Mungu katika historia ya watu wake. Moyo wa Bikira Maria ulikuwa makao ya Mungu, mahali pa kwanza ambapo Yesu alizaliwa. Kulingana na Wazee wa Kanisa, “Kabla ya kumzaa Yesu tumboni mwake, Maria alimzaa moyoni mwake.” Kwa hivyo haikuwa ngumu sana kwake Mariamu kuishi ushirika wa kina na moyo wa mwana wake Yesu. Mbele ya mateso ya Mwana, tunaitafakari huruma ya Mama, anayejua jinsi ya kupenda na jinsi ya kuteseka kwa ajili ya yule anayependa. Maria alichukua katika moyo wake uchungu wote wa mwanawe. Hivyo utabiri wa Simeoni hekaluni ulitimizika, yaani, alipochukua mtoto Yesu mikononi mwake, alimwambia mamaye, “Upanga utachoma moyo wako mwenyewe”.       


      Kati ya tabia kadhaa za Bikira Maria tukaribisheni ushuhuda wake wa ukimya kama mwanafunzi wa kwanza na mwaminifu wa Mwanawe. Yeye alichukua jukumu lake hadi matokeo ya mwisho. Wakati wanafunzi wengine walienda zao, Maria akabaki amesimama kando ya msalaba. Hebu mfano huu wa Maria utuimarishe ili tuweze kuishi kwa uaminifu utambulisho wetu kama wanafunzi wa Mwana wake Yesu na tujifunze jinsi ya kujitolea kabisa kwa wema wa engine.   

Fr Josuel Ndega
Mapitio na marekebisho: Sarah

Nenhum comentário: