terça-feira, 3 de maio de 2016

KUISHI KAMA MAKAO YA UTATU MTAKATIFU


Kutafakari kutoka Mdo 15,1-2.22-29; Ufu 21, 10-14.22-23; Yoh 14, 23-29

     Ujumbe muhimu wa liturjia ya siku ya leo ni kuhusu hali ya makao ya Mungu ulimwenguni na ndani ya kila mtu kupitia upendo. Hali hii inatualika kufanya upya ahadi zetu za waliobatizwa na kuboresha uhusiano wa kweli na yule ambaye anapendezwa kukaa ndani yetu. Hali ya somo la kwanza inaongea kwamba mwanzoni mwa uinjilishaji wanafunzi wa Yesu walihitaji utambuzi sana watangaze habari njema ya Yesu bila kipimo na masharti. Baadhi ya desturi za binadamu ni kama mzigo katika uhusiano wa watu na Mungu. Mazungumzo ya Pulo na Barnaba pamoja na mitume wengine wameongozwa na Roho Mtakatifu ni mfano wazi kuhusu njia ya Kanisa ya kutenda ili liweze kutatua shida na ugumu miongoni mwa wana wake kwa sababu ya tofauti ya tamaduni, ya mawazo na kadhalika. Kulingana na mtazamo wa Yohana, Mungu alifanya makao duniani na kupitia Yesu, aliye hekalu la kipekee tunaweza kukutana na Mungu kwa kweli. Mwelekeo wa safari yetu kama watu wa Mungu ni kushiriki katika utukufu wake na kutiwa nuru kupitia Mwana wake ambaye ni mwanga wa ulimwengu.

      Katika injili tuko na hotuba ya kuaga ya Yesu anayewashauri wafuasi wake walishike neno lake kama alama ya upendo wao kwake. Wanafunzi wana maana nzuri ya kufanya hivyo kwa maana hiyo ni njia maalum ya kuwa makao ambapo Utatu Mtakatifu wanaweza kuja na kukaa. Uhusiano wa ushirika kati ya Mwana na Baba na Roho Mtakatifu ni mwaliko wa ushiriki wa wale watakaoendeleza kazi ya Yesu ulimwenguni. Kipimo cha mwendo huu ni neno lake linalo asili katika Baba na linapatikana katika nyakati zote kupitia tendo la Roho Mtakatifu. Roho huyo ni msaadizi anayeweza kubadilisha maisha ya yeyote anayejifungua kwa tendo la neema ya Mungu. Wanafunzi wanaalikwa kuishi hatua mpya katika safari yao na maneno haya ya Yesu ni faraja inayoijaza mioyo yao kwa  matumaini. Yesu anawafundisha kwa uvumilivu jinsi ya kuishi utambulisho wa wanafunzi na kumkaribisha nyakati zote. Ingawa tangu mwanzo wa kazi yake Yesu alijifunua kupitia hali ya kawaida, mpaka hapo wanafunzi wake walikuwa na mazoea ya kumtambua Yesu kupitia mambo makuu. Kutoka hapo, wanapaswa kumtambua Yesu na kumdhihirisha kwa njia tofauti kabisa.

     Yesu atatoweka kimwili lakini ataendelea kwepo ndani ya wanafunzi wake kupitia upendo. Mahali ambapo Yesu yupo vivyo hivyo Baba na Roho Mtakatifu wapo. Ikiwa mara iliyopita (Yoh 13, 31-35) tulitafakari kuhusu haja ya kupendana kama Yesu alivyopenda, yaani, amri ya kupendana kama kipimo ili watu watambue nani ni kweli wanafunzi wa Yesu, sasa umuhimu wa kutafakari kwetu ni upendo kati ya Yesu na wanafunzi wake ambayo ni njia ya kweli ya kumfanya Mungu atambuliwe kwa wote baada ya kifo cha Yesu. Yesu hakuwaacha wanafunzi wake kama walio yatima bali ataendelea miongoni mwao kwa njia tofauti. Yeye, pamoja na Baba na Roho Mtakatifu wanakuja daima kwetu na kutarajia kukaribishwa vizuri. Ujio wao ni ufanisi sana, kulingana na Baba wa Kanisa Gregori, yaani, “wanakuja kwetu twende kwao; wanakuja kusaidia wakati wa dhiki; tunakwenda kwao kwa kutii; wanakuja kwa kutuelimisha, tunawaendea kwa kutafakari; wanakuja kwa kutujaza, tunawaendea kwa kushikilia; ufunuo wao si wa nje bali wa ndani; makao yao kwetu si ya muda bali ya milele. Imesemwa tutakuja kwake na kufanya makao kwake.”  


       Yesu anaongea kuhusu Baba kwa hamu na kutambua sana msaada wa Roho Mtakatifu katika kazi yake. Huu ni mwaliko wa tuishi uhusiano mpya miongoni mwetu hata tufikirie wengine muhimu kuliko sisi wenyewe na kutambua kazi yao muhimu zaidi kuliko zetu. Ufunuo wa Yesu unaleta changamoto kwetu tulioalikwa kuendeleza kazi yake. Alitaka kwamba kupitia maneno na matendo yetu dunia itamjue. Bila shaka kwamba tunapaswa kuwa waaminifu na mwendo huu ni matokeo ya kulisikia na kulishika neno lake ambalo ni kipimo cha upendo wetu kwake. Wakati tunalishika neno lake Yesu tunaruhusu kuingia kwa Utatu Mtakatifu ndani yetu. Hali hii tumeona tangu ubatizo wetu, lakini tumekosa ahadi ya kuishi kulingana na uwepo huu. Kuhusu hayo Mt. Paulo anatukumbusha haja ya heshima kwa miili yetu kwa sababu hii ni hekalu la Roho wa Mungu. 

Fr Ndega

Nenhum comentário: