quarta-feira, 20 de julho de 2022

TUISHI YALE TUSALIYO!

 

Kutafakari kutoka Lk 11, 1-13




 

    Baada ya kusema ni nini inapaswa kuwa kipaumbele maishani mwetu, siku ya leo Yesu anatufundisha jinsi ya kusali na kwa nini kusali. Basi, tunataka kutafakari kuhusu thamani kubwa ya sala ya Bwana, yaani, “Baba Yetu” na ahadi ambayo tunaalikwa kuchukua kutokana na sala hii. Kama muhtasari wa njili sala hii inadhihirisha utambulisho wa wakristo nasi tunaposali, tunataka kumaanisha kwamba sisi ni wamoja na wana wa familia moja, yaani familia ya watoto wa Mungu.

    Kupitia sala Yesu aliwapa wanafunzi wake mfano muhimu wa kuishi kwa sababu kwake kusali kulikuwa tabia yake ya kawaida. Katika mazungumzo hayo kutoka moyo kwa moyo, Yesu anamwita Mungu kama “Aba” na kuishi kwa uhusiano wa kina naye, kweli kama mtoto mdogo na baba yake. Basi, kusali ndivyo hivyo, uhusiano wa baba na mwana. Tunaposali tunahisi Mungu karibu sana nasi. Sala inaufungua moyo wetu kwa kuzitambua na kuzipokea zawadi zake. Ikiwa hatusali imani yetu inakuwa dhaifu daima. Ingawa wanafunzi wa Yesu walijua sala nyingi za dini yao nafsi yao ilihitaji uhusiano wa ndani. Walipomwona Mwalimu kusali waligundua mara njia kamili ambayo ilikosa kwa sala yao. Hivyo mmojawapo alimwambia, “tufundishe!”  

    Wakati Yesu alipowafundisha wanafunzi wake kusali, aliwakabidhi maneno aliyotokana na uhusiano wake na Baba na kuwakumbusha kuhusu haja ya kuwa na tabia kamili, yaani tabia ya mwana anayemwomba Baba kwa imani. Hii ni tabia ya kujisalimisha mikononi mwa Huyo anayejua mahitaji ya wana kabla ya wamwombe kitu. Yesu hakuhitaji kusali kwa sababu ni Mungu aliye mmoja na Baba; hata hivyo, alisali sana. Kwake mtu anapaswa kusali sio tu anapohitaji bali kwani hii ni sehemu muhimu ya maisha yake, kama vile kula chakula, kunywa maji ama kupumua.

    Sehemu ya kwanza ya sala hii ni utambulisho wa ubaba wa Mungu, ambao unaonyeshwa kupitia utunzaji na wema wake. Huu ni mwaliko wa kulitukuza jina la Mungu, yaani, “Baba yetu… jina lako litukuzwe!” na mambo yote yakujayo baada ya maneno “Baba yetu” yanayategemea maneno haya. Kulitukuza jina la Mungu ni kumpa Mungu utukufu wake kwa kufanya mapenzi yake kama Yesu alivyo, hasa aliposema “Chakula changu ni kufanya mapenzi ya Baba yangu.” Ni lazima kufanya mapenzi ya Mungu ili Ufalme wake utokee duniani kama mbinguni.

    Tunapaswa kumwelekea Baba huyo kwa imani kwa kuwa na uhakika kwamba tumepokea sana. Ni muhimu pia kuwa na uvumilivu na kuusubiri wakati wa Mungu. Tunaomba kwa ajili ya mkate na ya msamaha na ya upatanisho na ulinzi. Kulingana na Maandiko matakatifu, “kutokana na wema wake tumepokea neema juu ya neema”. Ushuhuda huu ni uthibitisho wa utunzaji wa upendo wa Mungu anayeshiriki zawadi zake na wana wake, kwa kutarajia kwamba tufanye vivyo hivyo kwa ajili ya wengine ili undugu kati yetu uwe maonyesho ya ubaba wake.

    Tunaposala Sala Baba Yetu tunaonyesha kwamba tunafikiria sio mahitaji yetu tu bali ya wengine pia. Sala hii inatufundisha kuomba kwa ajili ya lililo muhimu sana, yaani, “mkate wa kila siku”, kwa sababu tunapaswa kupigana na kila aina ya ukusanyaji na ubadhirifu wa chakula ambao unauharibu undugu, kwa kuwafanya maskini na wenye njaa wateseke. Kuhusu mambo haya Baba Mtakatifu Francisco asema: “Ulaji umetuongoza kutumia chepesi pamoja na ubadhirifu wa chakula cha kila siku... Tunapaswa kukumbuka kwamba chakula ambacho sisi hutupa takatakani ni kama tulikuwa tumeiba kutoka meza ya walio maskini na wenye njaa.”

Kwa Mt. Yohana Calabria, sala “Baba Yetu ni Injili kwa ufupi. Matatizo yote yapaswa kufikiriwa na kusomeka kwa maelewano na ubaba wa Mungu.” Ikiwa tunasema “Baba Yetu” ni kwa sababu tunasadiki kwamba sisi ni ndugu wa wengine wengi. Mungu hawabagui watu na hamsahau yeyote wa wana wake. “Kikundi chochote cha kidini kinapoanza kufikiri na kutenda kama kwamba Mungu yuko nao tu na sio watu wengine huko ni kumbinafsisha Mungu.” Sala kama hivyo haiwezekani kumpendeza Yeye kwa sababu haiwafikirii ndugu wengine.

Katika sala yetu mara nyingi hatupokei yale tunayoomba. Ni kwa sababu gani? Labda hatuombi ipasavyo. “Mstari wa mwisho wa injili hii unaonyesha nini cha kuomba na nini tutakachopewa, yaani Roho Mtakatifu”. Ndiye Yeye zawadi kubwa ambaye Baba anatupa naye anasali ndani yetu ili tusali kwa njia kamili. Roho huyo anatuhakikishia kwamba “sala ya kweli haimlazimishi Mungu kuyabadili mawazo yake ili ayafanye mapenzi yetu.” Basi, Mungu hatupatii daima yale tunayomwomba, bali anatupatia daima tunayohitaji, kulingana na mapenzi yake. Pamoja na kuwa njia ya kusali sala ya Baba Yetu ni njia ya kuishi. Tunaalikwa kuishi kwa undugu kutokana na uzoefu wa ubaba wa Mungu na kuwa na tabia kamili katika ushusiano wetu naye, yaani kuwa na tabia ya wana, kwa sababu mtu ambaye haishi kama mwana hapati kutenda kama ndugu. Roho Mtakatifu atusaidie kuishi maneno ambayo tunayasema tunaposali “Baba Yetu.”


Fr Ndega

Nenhum comentário: