sábado, 9 de janeiro de 2016

“WEWE NI MWANANGU MPENDWA, NIMEPENDEZWA NAWE”


Kutafakari kuhusu Isa. 42:1-4, 6-7; Mdo. 10:34-38; Lk 3: 15-16, 21-22

        Tunasherehekea sikukuu ya ubatizo wa Bwana Wetu Yesu Kristo. Hii ni nafasi maalum ya kuukumbuka ubatizo wetu na kuweka upya ahadi ya kuwa wakristo, kuishi wito wetu wa wana wa Mungu kama Kristo alivyo. Yeye ni mtumishi wa Bwana, katika somo la kwanza, aliyeitwa awe “agano la watu na nuru ya mataifa; kuyafunua macho ya vipofu, kuwatoa gerezani waliofungwa, kuwatoa wale walioketi gizani katika nyumba ya kufungwa.” Kulingana na kitabu cha Matendo, Yesu alifanya kazi njema kwa maisha ya watu kwa sababu Mungu alikuwa pamoja naye. Vivyo hivyo ni maisha mapya ya sisi sote tuliobatizwa katika Kristo, yaani tunakuwa Kristo tena, kwendelea utume wake kwa manufaa ya Kanisa lake na wokovu wetu kwa sababu yeye yuko pamoja nasi. Tumshukuru Mungu kwa zawadi ya ubatizo wetu ulio ushiriki katika uhai wake.

       Injili inatusaidia kukumbuka kitu kuhusu Yohana na kazi yake. Ukuu wa Yohane ulikuwa kutambua ukuu wa Bwana, akijifikiria mwenyewe kama sauti tu na asiyestahili kuulegeza ukanda wa viatu vyake. Yesu mwenyewe alitambua ukuu wa Yohane akiweka unyenyekevu wake kama mfano kwa safari yetu. Yohana aliwabatiza watu kwa maji kama kielelezo cha kugeuka kwao. Kupitia ishara hii alitangaza huruma ya Mungu iliyopatikana kwa wote. Basi ishara ya Yohane ilikuwa kielelezo cha kupita kutoka katika dhambi na mauti kwenda katika neema na maisha mapya ya Mungu. Jambo muhimu katika tendo hili la Yohana ni kwamba aliwabatiza wale waliomhitaji Mungu na kutubu dhambi zao. Yohane na watu hao waliamini kwamba ni Mungu anayesamehe dhambi zao. Lakini Yesu hakuwa na dhambi, kwa nini alibatizwa?

      Kwa Yesu ilikuwa nafasi maalum ya kuonyesha mshikamano wake kuhusu kazi ya ajabu ya Yohana, kuthibisha kwamba Mungu anatarajia kwamba watu ambao ni wake warudi kwake. Kama inatokea katika somo la kwanza, kabla ya Yesu kuongea na watu kwa mamlaka aliyoipokea kutoka kwa Baba, Mungu mwenyewe alimjulisha akisema: “Wewe ni Mwanangu mpendwa, nimependezwa nawe”. Sauti hii itasikika tena katika tukio la milima. Huko milimani Mungu Baba alionyesha pendo lake kuhusu Mwanawe na kuwaalika wote wamsikilize. Yesu alionyesha pia unyenyekevu akijifananisha na binadamu ambaye ana udhaifu na kuhitaji kuishi katika ushirika na Mungu. Yesu alikuja si kuishi kujitengwa na watu bali aishi kuhusishwa katika safari yao. Kabla ya Yesu maji yalikuwa na nguvu ya kutakasa mwili pekee yake. Kutokana na uzoefu huu Yesu aliyatakasa maji ili yawe na nguvu ya kutakasa pia roho ya watu, yaani maji ya ubatizo.


      Baada ya kupokea ubatizo wa Yohana na kujulishwa kama Mwana mpendwa wa Mungu Yesu aliwezeshwa na Roho Mtakatifu ili aanze kazi yake akipendekeza uzoefu huu kwa wote ambao wanataka kuwa watoto wapendwa wa Mungu. Tunaweza kusema kwamba ubatizo ambao Yesu anapendekeza ni uwezo wa kushiriki katika uzoefu wake wa Mwana wa Mungu. Ubatizo huu ni ishara ya utambulisho wa kikristo, yaani Ubatizo wa Roho Mtakatifu na kwa moto, kulingana na maneno ya Yohane Mbatizaji. Ubatizo huu una nguvu ya kufanya mabadiliko katika maisha ya mtu yeyote kwa sababu unamfanya kuzaliwa katika familia ya Mungu. Alama yetu kama watoto wa Mungu haiwezi kufutika. Ipo daima! Tunaweza kuishi maisha mapya ambayo ni zawadi ya Kristo mwenyewe na matokeo ya utume wake. Ubatizo wetu, pamoja na maondoleo ya dhambi, unadhamini ushiriki katika uzima wa Mungu mwenyewe. Kupitia alama hii ya nje tunakufa kweli kwa maisha ya dhambi, na pia tunapitia ufufuko wa maisha mapya katika Kristo aliye mshindi dhidi ya dhambi na mauti. Yeye ni mwanga wa kweli ambao unamtia nuru kila mtu. Yeyote akimfuata hatatembea gizani bali atakuwa na nuru ya milele. Kupitia mwendo huu tumekuwa wana wa nuru ili tutembee katika mwanga wa Mungu kila siku ya maisha yetu. Ekaristi hii itusidie kuishi lengo hili la safari yetu ya kikristo, walio wana wapendwa wa Mungu.

Fr Ndega
Mapitio: Sara

Nenhum comentário: