quinta-feira, 30 de março de 2017

MUNGU WA YESU KRISTO NA “PICHA” ZETU ZA MUNGU


Tafakari tarehe 1 Sam 16,1b, 6-7,10-13a; Eph 5,8-14; Jo 9,1-41


     Mungu ambaye Yesu ulionyesha ndiye Mungu wa huruma, Mungu aliyeshughulika na maisha ya binadamu, Mungu wa upendo, Mungu aliye Baba. Lakini mara nyingi tumesikia kwamba “Mungu anaadhibu;” au “Mungu analazimisha kwamba jambo lifanyike kwa njia moja na siyo ya nyingine; au kwamba mtu alimwua mwingine “kwa jina la Mungu;” au mbele ya hali mbaya, mtu anasema “ndiyo mapenzi ya Mungu,” n.k. Je, Mungu huyo tunayezungumzia ni Mungu mmoja aliyefunua Yesu Kristo? Nadhani wakati wa kupata kumjua Mungu vizuri umefika. Hakika “tunajua” mambo mengi kumhusu Mungu kwa njia ya akili; lakini ni lazima “kumjua” hasa kwa njia ya imani. Ninaongea juu ya kitenzi kujua kulingana na hali ya kibiblia, yaani uhusiano wa upendo. Baadhi ya namna za “mapepo” - picha za Mungu – tunaweza kufukuza kwa sala nyingi peke yake.

     Andiko la kwanza anaongea juu ya uchaguzi na upako wa Daudi kama mfalme. Vipimo Vilivyotumika kwa ajili ya jambo hili ni kinyume na matarajio yote ya kibinadamu. Kwa kawaida sisi tunapomtazama mtu tunaangalia hali ya nje ya mwili na kuzingatia nguvu zake; tena tunafikiria uwezo wa kuongea na mambo mengine ambayo yanasababisha mshangao kwetu – hayo ni mambo ya nje tu. Macho ya Bwana yanalenga yule aliye mdogo, asiye na umaarufu na yule mnyenyekevu. Mungu anaona vizuri kwa sababu anaweza kuona linalotokea moyoni mwa watu. Kwa hiyo, mtu anaweza kuona vizuri ikiwa anaweza kuona kama Mungu anavyoona na kisha, tena anaweza kutenda kulingana na moyo wake Mungu. Tunajua kwamba moyo ni mahali muhimu pa maamuzi yetu. Hivyo, ndipo moyoni tunapoamua kuishi kama watoto wa mwanga au watoto wa giza.

      Lakini kabla ya uamuzi wowote, Mt. Paulo anataka tufikirie kwamba tumeangazwa na Kristo ili tuwe na kuisha kama watoto wa mwanga. kwa upande wake, Mungu anatuhakikishia hali ya mwanga, lakini mwendelezo wa hali hii unalitegemea jibu la kila siku. Mimi najiguswa sana na maneno ya Mtakatifu fulani ambaye anasema, “Je, sisi tu ni nani? Sisi tu watoto wa Mungu; na tena, Je, tunakuwa nini? Hili ni jibu letu kwake.” Bila shaka kwamba katika majibu yetu haiwezekani kukosa matunda ya wema, haki na ukweli. Ni vizuri kujua kwamba Mungu ana mpango wa upendo kwa maisha yetu na tena anatupa zawadi zote kwa kutimiza mpango huu. “Yeye anatuambia kwa nabii Yeremia: Je, Efraimu si mwanangu mpendwa, mtoto ninayependezwa naye? Ingawa mara kwa mara ninanena dhidi yake, bado ninamkumbuka. Kwa hiyo moyo wangu unamwonea shauku, nina huruma kubwa kwa ajili yake (Yer 31.20).”

       Katika Yesu, Mungu ana njia maalum ya kuangalia. Yesu anaona mtu aliyezaliwa kipofu na mtazamo wake umejaa upole na huruma. Wakati wengine waliangalia na kumwona mtu aliye na hatia na kuadhibiwa na Mungu, Yesu alimwona mtoto mpendwa wa Mungu, ambaye ana hamu kubwa ya kushiriki kikamilifu katika jumuiya na kuwatambua wengine kama ndugu na dada wa kweli. Swali la wanafunzi linaonyesha mawazo ya mazingira yale ambayo yalifikiria upofu na magonjwa mengine kama adhabu ya Mungu. Yesu hakujibu nini iliyousababisha upofu. Yeye alipendelea kufunua picha ya kweli ya Mungu akiwatunza watu kwa njia ya pekee. Akimponya mtu aliyezaliwa kipofu, Yesu alidhihirisha pia utambulisho wake kama Masihi, kwa sababu kulingana na utabiri wa nabii Isaya Masiha aliyetarajiwa peke yake aliweza kufanya tendo kama hilo (Isa 29:18). Hivyo, maana ya maswali ya Mafarisayo na upinzani wao wa kukubali kwamba tendo hili litoke kwa Yesu.

    Yesu anajifunua kama mwanga wa ulimwengu na kuhakikisha kwamba wale wanaomfuata hawatembei gizani, bali watakuwa na mwanga wa uzima. Kumfuata Yesu ni kutembea katika mwanga. Na kufuata huku hufanyika katika mwendo wa kuangazwa kama ilivyotokea kwa uponyaji wa kipofu yule. Mate ya Yesu yalichanganywa na ardhi yalisababisha hali mpya. Ndio uumbaji mpya kwa yule kipofu kama ilivyotokea katika mwanzo wakati Mungu Alipomwumba mtu kwa udongo na kwa pumzi yake alimletea binadamu uhai. Mate ya Yesu ni ishara ya Neno lake linalotupa mtazamo mpya na hamu ya kutembea. Lakini kutambua kazi hii ya neno lake haitoshi kuwa mwanafunzi wake. Tunapaswa kumtambua yeye kama mtu aliye zaidi ya “binadamu aliyeitwa Yesu” na zaidi ya “nabii.” Yeye ni Kristo wa Mungu naye anataka kujifunua mwenyewe anapokutana na kila mmoja wetu kwa njia ya kibinafsi ili tuweze kumtambua na kumshuhudia. Ndiyo katika sala daima ambayo inatokea utambulisho wa mwanafunzi na Mwalimu wake.


        Kutokana na mwendo huu tunaweza kuchukua mambo matatu muhimu kwa safari yetu. Kwanza, ni kuhusu mtazamo wetu juu ya Mungu. Tunahitaji kurekebisha picha zetu za Mungu. Ndilo kosa kubwa kufikiri kwamba tunaweza kudhibiti Mungu na vipimo vyetu vidogo vidogo. Hatuwezi kuweka mipaka kwa ukarimu wake na huruma yake. Kile tunachohitaji kwa kweli ni kuruhusu Mungu awe Mungu na kutufunulia kwa nguvu zote za upendo wake. Pili, ni kuhusu maono yetu juu ya wengine. Tunapaswa kujifunza kuangalia kwa “mtazamo” wa Mungu, kwa sababu tuna maono yenye upungufu. Wakati tunapoangalia watu sisi huwahukumu na hata tunawaadhibu. Mtazamo wa Mungu hauhukumu wala hauadhibu, bali unamsukuma mtu aende mbele kwa sababu huu ni mtazamo wa upole na huruma. Tatu, ni kuhusu haja ya ushirika kati ya tamani yetu na mapenzi ya Mungu. Mapenzi yake ni “kutubadilisha ili tuwe kama Mwana wake Yesu.” Huu ni mwendo wa muda mrefu unaotokea kila siku kwa kusikiliza Neno lake ambalo linatuita kutubu, linagusa mioyo yetu na kutuimarisha tutende mema.” Hivyo, hatua kwa hatua, tutaponywa juu ya mtazamo wetu wenye upungufu kuhusu Mungu, kuhusu sisi wenyewe na kuhusu wengine.

Fr Ndega

Nenhum comentário: