domingo, 12 de fevereiro de 2017

THAMANI YA MANENO YETU


Kutafakari kuhusu Eclo 15,15-20; 1Cor 2,1-10; Mt 5,17-37

       Mungu anayaongoza mambo yote duniani kulingana na mpango wake wa hekima na wema. Hakuna lolote ambalo linakosa mtazamo wake wa upendo. Yeye anauheshimu uhuru wa wanadamu naye anapopendekeza kwao njia ya kupata uzima, anatarajia waweze kuchagua vizuri na kuishi milele. Kulingana na Paulo, hekima ambayo ilikuwepo na Mungu tangu milele imo ndani yetu na kutuongoza katika maamuzi yetu. Fumbo hili Mungu aliwaandalia wanaompenda na kutufunulia kwa Roho Mtakatifu. Kutambua hili ni sharti ili tuweze kufanya tofauti katika hali zetu.
        Injili ya Mathayo inamjulisha Yesu kama “Musa mpya” na mafundisho yake ni mapya kabisa. Hatuwezi kusema kwamba kuna kupasuka kati ya mafundisho yake na yale ya mababu wa zamani, bali mwendelezo. Lakini, ingawa hayo ni mwendelezo, ndiye Yesu anayetafsiri kwa njia kamili mambo yote yaliyosemwa. Kwa hivyo, aliwaalika wasikilizaji wake wamsikilize akisema, “Lakini mimi nawaambieni...” Alisema hayo kwa sababu alikabiliana na ugumu wa mioyo ya baadhi ya watu. Hata hivyo, aliyaheshimu maandiko ya Agano la Kale na tena aliwashauri watu wayaheshimu maandiko hayo. Basi Agano la Kale linaendelea kuwa muhimu kwa Wakristo, kwa hivyo Yesu alisema kwamba Yeye hakuja kutangua Torati au Manabii. Kweli yeye amekuja kukamilisha ahadi zilizotolewa kwa njia ya maandiko haya. Yeye yu uthibitisho mkuu wa uaminifu wa Mungu kwa ahadi zake.
        Yeye “alitaka kurekebisha mambo makubwa zaidi,” akigundua tena mpango wa Mungu wa kiasili. Mpango huu ni ufunuo wa upendo wake ambao hawezi kuutegemea mtazamo wa kipungufu wa binadamu. Yesu anasisitiza kwamba haki ya wanafunzi wake inapaswa kuishinda ile ya Mafarisayo na Waandishi wa sheria. Katika Mathayo, haki inamaanisha mapenzi ya Mungu na wenye haki ni wale wanaofanya mapenzi yake. Mapenzi haya ni kwamba watu waweze kuishi ukarimu bila kipimo, wakifanya zaidi kuliko kuitii sheria, yaani, uhusiano wa heshima na upatanisho. Kidogokidogo wanafunzi wa Yesu walikuwa wakitambua kwamba matarajio ya Yesu yalikuwa kuanzisha uhusiano mpya kati ya watu na Mungu na tena miongoni mwa watu. Yeye anataka “watu wawe na utii unaotoka moyoni, na siyo utii wa unafiki kwa sheria tu za nje tu.”
       “Yesu anataka sheria zetu ziendane na matendo yetu. Utii wa sheria tu, pasipo matendo ya kweli, hauwezi kutusaidia lolote katika maisha yetu. Ni mioyoni mwetu, na kwa upendo kama wa Yesu, ndipo tutaweza kutimiza amri za Mungu kwa maneno na matendo”. Hivyo, ni Injili ya Yesu inayopaswa kuwa sheria katika uhusiano wetu wa kibinadamu. Ikiwa tunataka kuwa na uhusiano mwema na Mungu hatuwezi kuwapuuza wengine ama kuwa na uhusiano mbaya nao. Kulingana na mtazamo mpya wa Yesu,  njia ya mtu ya kuishi inaweza kusababisha mauti ya mwingine bila haja ya kutumia bunduki. Kuwa na hasira na mtu na kuionja hisia hii kwa muda mrefu ni kumwua mtu huyo moyoni mwako. Kwa Yesu hayo ni mauaji ya kweli. Kutoheshimu ni mwanzo wa mauaji hayo.
      Tunaalikwa kuwa macho kwa sababu kila wazo, neno na tendo ambalo halilengi kutimiza mapenzi ya Mungu kama alivyofikiri Yesu linampa yule Mwovu nafasi na kuharibu maisha yetu ya kifamilia na kijumuiya. Uhuru wetu unatuongoza kuyatumia maneno kama chombo cha kujenga undugu, mfano maneno ya upendo, ya faraja, ya tumaini, n.k.; au tena kama chombo cha kuharibu, mfano maneno ya dharau na ya uvumi. Uvumi kuhusu mtu fulani huondoa heshima yake. Kuna hadithi moja inayoyahusu mawazo ya Yesu na kutusaidia kushinda hali mbaya ya uvumi. “Siku moja mtu mmoja alimwendea Socrates mwanafalsafa wa Kigiriki na kumwambia, “sikiliza umbea juu ya rafiki yako.” Socrates alisema, “Ngoja, ujumbe unaotaka kunipa je umeupitisha kwenye vipimo vitatu?” Vipimo vitatu ni vipi?” Socrates alijibu, “Je unayotaka kuniambia ni ukweli?” Mtu huyo alijibu, “kusema kweli nimesikia toka kwa mtu mwingine.” “Je unayotaka kuniambia ni jambo la upendo?” Mtu huyo akasema, “Si la upendo hasa, kusema kweli ni kinyume.” Mwishowe, Socrates aliuliza, “Je ni jambo la lazima?” Mtu huyo alijibu, “Si lazima hata kidogo.” Socrates alimalizia kwa kusema, “kama jambo unalotaka kuniambia halina ukweli, si la upendo na si la lazima achana nalo.”

      Tunaalikwa kuongea kwa bidii kwa sababu maneno yanagusa ndani kabisa na kuongoza uhusiano wetu na Mungu na pia kati yetu. Ikiwa maneno yetu anasababisha uchungu kwa wengine, sharti kwetu ni upatanisho. Hatuwezi kuishi uhusiano wa kweli na Mungu wakati hatupatanishi na mtu ambaye tumemkosea au ametukosea. Kulingana na Yesu, ninapaswa kuchukua jukumu la upatanisho, hata ikiwa sina hatia. Nataka kumaliza kwa kutumia kitikio ya wimbo fulani kutoka Brazil: “Neno ni kama lulu ndiyo, yeyote anayejua thamani yake anaongea kwa bidii; neno ni kama moto ambayo inachoma hadi mwisho, yeyote anayejua yale anayosema atakuwa mwenye furaha mno.” 

Fr Ndega
Marekebisho: Serah Thuo

Nenhum comentário: