domingo, 8 de janeiro de 2017

MWANGA AMBAO UNATUONGOZA KWA MUNGU


Kutafakari kuhusu Is 60, 1-6; Ef 3, 2-3a. 5-6; Mt 2, 1-12

      Kidogo kidogo na hatua kwa hatua, liturujia imetusaidia kufahamu maana ya kuzaliwa kwa Yesu na nia ya Mungu kuhusu hali ya binadamu. Yesu alizaliwa katika Bethlehemu iliyo nchi ya Wayahudi, lakini sio kwa Wayahudi tu, bali kwa mataifa yote. Maelezo ya kuzaliwa kwake katika injili za Mathayo na Luka yanaonyesha kuwa tangu mwanzo wa maisha yake ya kibinadamu, Yesu alikataliwa na nchi yake, lakini alitafutwa na kuheshimiwa na wale wasiyo Wayahudi. Hali hii ni uwazi sana pia katika injili ya Yohane (1,11-12), ingawa injili hii haitoi maelezo kuhusu utoto wa Yesu kama injili zingine mbili zilivyo. Kulingana na Yohane, Yesu “alikuja katika nchi yake mwenyewe, nao walio wake hawakumpokea. Lakini wale waliompokea, wale waliomwamini, aliwapa uwezo wa kuwa watoto wa Mungu.” Basi, Yesu alikuja kwa wanadamu wote na kuwaangazia wote kwa mwanga wake. Kuzaliwa kwake kutuhakikishia kwamba wote ni watoto wa Mungu na kwamba ni mapenzi ya Mungu kuwaokoa wote.

      Somo la kwanza ni wimbo uliofanyika baada ya utumwa wa Babeli na kutangaza makuu ya Bwana kwa watu wake. Kwa ajili ya hali hii nabii Isaya anaona Yerusalemu ukibadilishwa kuwa ni rejeo la hija ya watu wengi. Kweli utukufu wa Bwana uliangaza juu ya mji huu, lakini maana ya mahali hii ni ya kiimani kuliko ya kijiografia. Katika mji huu Yesu alitimiza kazi yake kuwahakikishia wote wokovu wa Mungu. Basi, wazo wa wokovu ulikuwako katika Agano la Kale, lakini sio wazi sana. Tafsiri kuhusu hali hii ilikuwa ya kikabila na kitamaduni, wakifanya wokovu wa Mungu uitegemee mipaka ya dini na tamaduni za Kiyahudi. Hali hii iliwazuia Wayahudi wawakaribishe watu wengine na kuwafikiria kama majirani ama ndugu. Yesu alizaliwa kama mwanga kwa ajili ya kuwafanya wanadamu wote wawe familia moja. Katika waraka wake Mtakatifu Paulo anadhihirisha kuwa Yesu ndiye ufunuo wa fumbo ambalo lilifichika kwa muda mrefu. Kulingana na ufunuo huu Wasio Wayahudi ni warithi wa ahadi za Mungu pamoja na Wayahudi. Uwepo wa Yesu unatafsiri kwa njia kamili yote ambayo yalisemwa na Mungu kwa manabii wa zamani. Kwa kifupi, Mungu aliwachagua Watu wa Israeli kama chombo ili awafikie wengine wote kwa urahisi.

     Kweli habari ya kuzaliwa kwa Yesu ni njema, lakini makaribisho kuhusu habari hii hayakuwa sawa kwa wote. Kwa upande wa Wageni waliotoka Mashariki, habari hii ikaileta maana ya kweli kwa maisha yao; kwa hivyo walimtafuta mfalme mpya kwa hamu sana bila hofu ya kuacha nchi yao na usalama wao. Kwa upande wa viongozi wa Wayahudi habari hii ilisababisha wasiwasi na msukosuko kwa sababu walikuwa na hofu ya kupoteza msimamo na upendeleo wao. Ujio wa mamajusi uliutimiza utabiri wa nabii Isaya (60,3) unaosema, “Mataifa yataujia mwanga wako, wafalme waujia mwanga wa pambazuko lako.” Walimtolea Yesu zawadi za thamani kubwa kwa tamaduni zao, yaani, dhahabu, uvumba na manemane.” Katika zawadi hizi walionyesha utambulisho wa watu wao, utajiri wao, vipaji vyao, juhudi zao na matarajio yao. Mamajusi waliacha nchi zao na kujiruhusu kuongozwa na nyota ili wafikie mwelekeo kamili wa maisha yao. Nyota hii inamaanisha mwanga wa Mungu uliowaangazia watu ili wamtafute yeye kwa hamu. Tena mwanga huu ni Mwanawe mwenyewe ambaye haruhusu atembee gizani yeyote anayemfuata (Yoh 8,12).

        Siku ya leo Mungu anatualika kuwa macho kuhusu nyota anayotumia kutuongoza. Je, umegundua nyota ambayo inatoa maana ya kweli kwa maisha yako? Katika injili zote tunaweza kukuta ishara nyingi za nyota hii. Tuchukue kama mfano wavuvi waliovua samaki wengi; kwao samaki walikuwa ni nyota ya Yesu. Kwa wakulima mbegu zilikuwa nyota ya Yesu. Kwa bibi na bwana harusi huko Kana divai ni nyota ya Yesu kwa sababu muujiza wa maji kubadilika kuwa divai ulimtangaza Yesu. Kwa mwanamke aliyekuwa anachota maji, nyota ya Yesu ilikuwa ni maji. Kwa Petro aliyemkana, Yesu aliandaa moto ambapo aliweka samaki; moto ikawa nyota ya kumrudisha Petro kwa Yesu. Kwa wafuasi wake  wa Emmaus waliokata tamaa, mkate ulikuwa nyota ya Yesu. Walimtambua katika kuumega mkate. 

        Kama ilivyotokea na mamajusi, maisha yetu ni safari ya imani ili tukutane na Mungu na kuruhusu aweze kuzibadilisha njia zetu. Tunaalikwa kuacha baadhi ya mawazo na usalama usio kweli na kuanza safari ya kukutana na Mungu tukiongozwa na msukumo wake. Tunaalikwa kumtolea yeye muhimu ya maisha yetu kwa maana yeye anastahili. Zawadi ambazo tunaweza kuzitoa zinatokana na ukarimu wake mwenyewe. Huyo Yesu ambaye tunatambua kama zawadi kubwa ya Mungu kwetu anataka kuwa mwanga wetu daima ili tuwe nuru pia kwa ajili ya wokovu wa wanadamu wote.


Fr Ndega

Nenhum comentário: