quinta-feira, 11 de fevereiro de 2016

WAKATI WA MABADILIKO NA WA WOKOVU NDIO SASA


Kutafakari kutoka  Yoe 2, 12-18; 2Kor 5, 20-6:2 Mt 6, 1-6; 16-18

        Kwaresima ni siku arobaini za maandalizi kwa adhimisho la fumbo la Pasaka ya Kristo. Wakati huu unatukumbusha siku arobaini ambazo Musa alibaki milimani Sinai; pia miaka arobaini ya Wana wa Israeli jangwani; tena siku arobaini za Eliya akitembea mpaka milima Horebi na siku arobaini za Yesu jangwani aliyeongozwa na Roho Mtakatifu. Wakati wa kwaresima unalenga kuwa uzoefu wa jangwa. Kwa upande wa viongozi wengi katika biblia jangwa palikuwa mahali pa mkutano na Mungu kwa hamu na uzoefu wa utakaso. Walitafuta mahali huko kabla ya matukio muhimu maishani mwao ili waweze kuchukua ahadi kwa nguvu na uaminifu. Vivyo hivyo, ni Kwaresma kama maandalizi kwa tukio muhimu sana la imani yetu, yaani Ufufuko wa Yesu.   

       Ni wakati kwa kutafakari kwa njia ya ndani kuhusu huruma ya Mungu na hali yetu ya wenye dhambi. Hasa katika Mwaka huu wa Jubilei, kutafakari kwetu kuhusu huruma ya Mungu kunatuongoza kuishi katika mwanga wa maneno ya Bwana: “Muwe na huruma kama Baba yenu alivyo na huruma (Lk 6, 36).” Dhamiri kuhusu matokeo ya dhambi katika maisha yetu inatuongoza kumwomba Mungu kulingana na somo la kwanza, yaani “Wahurumie watu wako ee Bwana!” nasi tunajua kwamba Mungu anawahurumia watu wake sio kwa sababu wanastahili, lakini kwa sababu hii ni tabia yake ndiye mwenye neema, amejaa huruma; si mwepesi wa hasira, bali ni mwingi wa rehema. Kulingana na Baba Mtakatifu Francisco, “Mbele ya ukubwa wa dhambi, Mungu anajibu kwa msamaha kamili. Huruma itakuwa daima kubwa kuliko dhambi yoyote, na hakuna awezaye kuuwekea mipaka upendo wa Mungu anayesamehe daima.” Kwa hivyo tunaalikuwa kumrudia yeye kwa imani na kuutumainia wokovu wake. Kama mwendelezo, somo la pili linaongea kuhusu mahitaji ya upatanisho na Mungu kwa sababu yeye mwenyewe anatupa nafasi ya kufanya hivyo kwa njia ya Mwanae Yesu Kristo. Huu ni wakati wa neema, nasi hatuwezi kuipokea neema ya Mungu bure. Wakati wa mabadiliko na wa wokovu ndio sasa.

     Katika dini ya kiyahudi, kuna hatua tatu muhimu sana ambazo zinadhihirisha utambulisho wa myahudi wa kweli, yaani sala, sadaka (itolewayo kwa maskini) na kufunga. Hasa wakati huu wa kwaresima tunaalikwa kuchukua hali hizi kama ishara ya toba yetu. Yesu alipopendekeza hatua hizi tatu, yeye aliwakumbusha wafuasi wake kuhusu maana na roho ambayo lazima kuimarisha hatua hizi. Wakati wa Yesu, kufunga kulikuwa shughuli ya kawaida, naye pia alifunga kwa wakati wa siku arobaini jangwani kabla ya kuanza ujumbe wake kwa umma. Yesu alitaka kwamba wanafunzi watende kwa tabia ya kweli sio kama ile ya baadhi ya watu (wanafiki) ambao walipofunga wakaonyesha huzuni; hao walikunja nyuso zao wapate kuonekana kwa watu kuwa wanafunga. Yesu aliihakiki tabia hii na akasema kwamba wamekwisha pata tuzo lao. Kwa Yesu kufunga kuzuri ni kujinyima baadhi ya chakula kwa mshikamano na maskini. Tunaweza kueneza ujumbe huu kwa kufunga baadhi ya maneno, ya matendo na ya mawazo ambayo si mazuri katika uhusiano wetu na wengine. Kwa hivyo kanisa katoliki linapendekeza hayo hasa wakati huu ambao ni kipindi maalum cha toba na mabadiliko ya maisha.


         Kuhusu sala, ni vizuri pia kuufuata mfano wa Bwana wetu. Yeye alikuwa mtu wa sala na aliijulisha sala kama njia ya uaminifu kwa mpango wa Mungu. Sala yake ilikuwa maonyesho wa uhusiano wake na Baba na mwaliko kwa wanafunzi wake wafanye vivyo hivyo kama utambulisho naye. Kwaresima ni wakati wa sala kwa hamu zaidi, kufungua akili zetu na mioyo yetu kwa tendo la wokovu wa Mungu. Huu ni wakati pia wa kutenda matendo ya huruma kwa wenzetu, kuonyesha juhudi yetu ya kubadili hali yetu na kandokando yetu. Majivu usoni ni ishara ya hali yetu ya ndani na kwamba tunakubali mwaliko wa Kanisa wa toba kwa sababu wakati wa kuukaribisha wokovu wa Mungu na kuiamini injili ndio sasa.   

Fr Ndega
Mapitio: Sara

Nenhum comentário: