domingo, 20 de dezembro de 2015

UTUMISHI NA UKARIMU WA BIKIRA MARIA


Kutafakari kuhusu 5,2-4; Waebrania 10, 5-10; Luka 1:39-45

      Liturujia ya jumapili hii inatujulisha mtu muhimu sana kama kielelezo cha matayarisho na makaribisho kwa Yule atakayekuja, yaani Bikira Maria. Mkutano wake na dada yake Elizabeti ni alama ya mambo makuu ya Mungu ambaye ana mtazamo maalum kwa hali ya wanyenyekevu na maskini. Kutokana na hali hii alidhihirisha fumbo la mapenzi yake. Anawatumia waliopatikana ili mipango yake yatimize. Katika somo la kwanza nabii Mika anatangaza kuzaliwa kwa mkombozi mmoja kwa Waisraeli atakayetawala milele kwa nguvu za Bwana. Yeye ni mfano wa mwokozi wetu Yesu Kristo aliyekuja kwa ajili ya ulimwengu wote akifanya mapenzi ya Mungu, kulingana na ujumbe wa Waraka kwa Waebrania. Kupitia kujisalimisha kwake mara moja tu tumepata utakaso na wokovu. 
    
     Alipoelewa mpango wa Mungu katika maisha yake Maria alijibu: “Mimi ni mjakazi wa Bwana, nitendewe kulingana na neno lako”. Hili lilikuwa jibu la ajabu la Bikira Maria mbele ya tangazo la Malaika Gabrieli. Wito wa Maria ni maonyesho ya ukarimu wa Mungu. Ukarimu wa Bwana ulihamasisha ukarimu wa mtumishi wake aliyeenda kwa haraka kutembelea dada yake Elisabeti ambaye pia alikuwa amepata mimba na alikaribia kuzaa kwani ilibaki miezi mitatu. Mkutano wa wanawake wawili ni mkutano wa agano, yaani Agano la Kale linalikaribisha Agano Jipya. Kuna pia mkutano wa vizazi, yaani mzee anamkaribisha kijana na kijana anamtumikia mzee. Mpango wa Mungu unajumuisha vizazi vyote na kila kizazi kinaalikwa kuchukua ujumbe wake kulingana na mwendo wake wenyewe. Tukio hili la wanawake hawa wawili linaonyesha njia maalum ya Mungu ya kutenda, dhidi ya matarajio ya binadamu, ni kwamba, mwanamke asiyezaa anakuwa mwenye rutuba na mwanamke bikira anapata mimba kwa njia ya ajabu.

    Maria alitaka kushiriki furaha ya Elizabeti kwa kuwa Mungu alikuwa ameingia katika maisha yake. Elizabeti na Yohana Mbatizaji ambaye alikuwa bado hajazaliwa wanashiriki pia furaha ya Maria na Yesu ambaye hajazaliwa. Wanawake wawili kukutana, watoto wao pia wanakutana. Maria anatukumbusha kwamba ni lazima kuondoka na kuenda kukutana na wengine na kuyatambua matendo ya Mungu maishani mwao. Maria anatusaidia kuamini kwamba matendo makuu ya Mungu katika historia ni ishara ya uaminifu wake. Tunaalikwa kuchukua ahadi ya kuondoka na kuenda kwa wengine kuona walivyobarikiwa na Mungu. Wengi wanangojea kutembelea kwetu na mshikamano wetu. Kwa kufanya hivyo tunahitaji kushinda baadhi ya vikwazo vinavyotuzuia kushirikiana na baadhi ya watu katika jamii au kabila jingine.


      Basi, ni mwenye furaha aliyeamini katika ahadi ya Mungu, kwa maana Yule anayeahidi ni mwaminifu. Imani inakuwa kigezo/kipimo cha msingi wa furaha. Maria anakuwa ishara ya ubinadamu mpya, uliobadilishwa na kuokolewa na Mwanae. Maria ni mmoja wetu ambaye alijihisi aliyeangaliwa kwa huruma na akaishi kwa shukrani. Aliyeangaliwa kwa huruma kwa sababu Mungu alitenda makuu maishani mwake. Yeye aliishi kwa shukrani kwa sababu aliyapatikana maisha yake ili, kupitia jibu lake, Mungu atende makuu maishani mwa watu hasa maskini. Kwa kiwangu kidogo sisi pia tunapitia tabia hizi, ni kwamba, tumeangaliwa kwa huruma kupitia zawadi kubwa ya wito. Tabia ya shukrani ndani yetu inaonyeshwa nje kupitia utumishi kwa furaha na ukarimu. Hali ya kuwa walioangaliwa kwa huruma haitutegemei sisi, bali inamtegemea Mungu ambaye anatujalia baraka nyingi; hali ya kuwa kama walio na shukrani inatutegemea sisi peke yetu. Mbele ya majaribio ya kufa moyo au kukata tamaa Maria ni kielelezo kwetu kwa upatikanaji kabisa kwa mipango ya Mungu. Kama yeye tunaalikwa pia kuishi kama wamebarikiwa na kumchukwa Yesu kwa wengine katika mahali po pote tuendako.   

Fr Ndega
Mapitio: Sara

Nenhum comentário: