quinta-feira, 17 de dezembro de 2015

MAANA YA UWEZO WA YOHANA WA KUWATHIBITISHIA WASIKILIZAJI WAKE


Kutafakari kuhusu Sef 3, 14-18; Wap 4, 4-7; Lk 3, 10-18

       Liturujia ya jumapili hii tatu inaleta mwaliko kwa furaha kwa sababu ya ukaribu wa ujio wa Bwana wetu. Hali hii tunaweza kutambua kupitia ujumbe wa nabii Sefania ambaye waliwahamasisha waisraeli wafurahi na kumshangilia Mungu mfalme wao. Maana ya furaha kubwa ni kwa sababu uwepo wa Mungu katikati yao ulileta ukombozi ukidhamini usalama na ulinzi dhidi ya maadui yao. Ujumbe wa furaha unaendelea pia kupitia waraka wa Paulo kwa Wafilipi kwa sababu Mungu yu karibu na neno lake ni alama ya ukaribu wake. Ukaribu wa Mungu ni uwepo wake kwa wakati sawa na uwepo wake ni ufanisi, yaani ni nafasi ya wokovu.
        Kuhusu injili tuna vipengele vingi kwa kutafakari kwetu. Andiko hili ni mwendelezo wa injili ya jumapili iliyopita. Luka anaendelea kueleza kuhusu kazi ya Yohane Mbatizaji na kipengele cha kwanza ni kuhusu uwezo wa Yohana wa kuwathibitishia wasikilizaji wake. Kama ilitokea na manabii wa zamani, tunaamini kwamba uwezo huu unatokana na uzoefu wa kweli wa Neno la Mungu. Yohane alifikiwa na Neno la Mungu jangwani. Yeye aliishi katika upweke wa jangwa, aliyefunguliwa kabisa kwa msukumo wa Mungu. Alijifunza kutokana na Neno la Mungu jinsi ya kuwa shahidi wa habari njema ya wokovu. Miongoni mwa wasikilijazi wa Yohane, Luka anawataja watoza ushuru na askari ambao walitaka kubatizwa. Hasa watoza ushuru walichukiwa na Wayahudi wenzao kwa sababu walikuwa washirika wa Roma. Wakati wa Yesu, watoza ushuru waliwekwa katika kundi maalum la wenye dhambi. Kuchanganyika nao kulimfanya mtu apate dhambi yao pia. Yesu alichanganyika nao, akivuka mipaka iliyowekwa na watu. Kikundi hiki pamoja na askari walitambua ukweli wa hali yao na hivyo wakaomba msamaha. Lakini nia njema pekee haitoshi. Yohane anawataka watende haki.  Kwa hivyo aliwaalika washiriki mali yao.
       Ukuu wa Yohane Mbatizaji ulikuwa kutambua ukuu wa Bwana, akijifikiria mwenyewe kama sauti tu na asiyestahili kuulegeza ukanda wa viatu vyake. Yesu mwenyewe alitambua ukuu wa Yohane akiweka unyenyekevu wake kama rejea. Hatuhitaji kumlinganisha Yesu na Yohane Mbatizaji ili tugundue ni nani kati yao ni mtu mkuu. Bila shaka Yesu ni mkubwa zaidi kuliko Yohane. Lakini ni vizuri sana kutambua uhusiano huu wa ajabu kati ya wote wawili. Ikiwa Yohane anaongea kuhusu Yesu anamsifu; ikiwa Yesu anaongea kuhusu Yohana anafanya vivyo hivyo. Tunahitaji kujifunza sana kutokana na uhusiano huu, kwa manufaa ya Kanisa na kwa wema wa uhusiano wetu kama wakristo, watumishi wa mwili wa Bwana.
         Basi, ni kazi ya Yohane kutangaza mwisho wa wakati wa kumgojea Masiya na mwanzo wa historia mpya, ambayo ilifanywa na watu wapya waliofanywa upya katika Roho wa Kristo. Kama huu ni uzoefu wa ubatizo. Lakini ni lazima kukumbuka baadhi ya tofauti kati ya ubatizo uliotolewa na Yohane na ule atakaotoa Masiya. Yohana aliwabatiza watu kwa maji kama kielelezo cha kugeuka kwao. Uzoefu huu ulikuwa hatua muhimu, bali haikufikia mabadiliko kamili ya ndani. Ubatizo wa Roho Mtakatifu na moto una nguvu ya kufanya mabadiliko kwa sababu unamfanya mtu kuzaliwa katika familia ya Mungu. Alama yetu kama watoto wa Mungu haiwezi kufutika. Hii ni chapa ya ubatizo wetu. Ipo daima!

        Wakati wa Yohane Mbatizaji unaomhusu Kristo ni mwendelezo, lakini unaushinda wakati wa maandalizi wa zamani. Huu ni wakati wa kutangaza kuhusu mahitaji ya kumkaribisha Bwana aliyetaka kukutana na binadamu. Basi kwa upande wa Mungu, mwendo wa mkutano uko tayari. Kwa upande wa binadamu ni lazima imani na kukubalika kwa uhuru na binafsi. Ikiwa ukuu wa Yohana ulikuwa kutambua ukuu wa Bwana, ukuu wa kila mtu katika ufalme wa Mungu ni kuyakubali mapendekezo ya Yesu na kuzifuata nyayo zake. Kielelezo cha Yohane kiwe daima rejea kwa safari yetu ya kukubalika kwa mipango ya Mungu na kuutangaza wakati wa kutembelea kwake kwetu daima. 

Fr Ndega

Nenhum comentário: