domingo, 14 de agosto de 2016

BABA YETU ANATUPA ROHO MTAKATIFU


Kutafakari kutoka Lk 11, 1-13

       Siku hii ya leo tunataka kutafakari kuhusu thamani kubwa ya sala ya Bwana, yaani, “Baba Yetu” na ahadi ambayo tunaalikwa kuchukua kutokana na sala hii. Ingawa tunatumia maneno haya, yaani, “Sala ya Bwana”, tusisahau kwamba hii ni sehemu muhimu ya utambulisho wa wakristo nasi tunaposali, tunataka kumaanisha kwamba sisi ni wamoja na wana wa familia moja kwa sababu Mungu ni wa wote. Kwanza kabisa Yesu akisali aliwapa wanafunzi wake mfano muhimu wa kuishi kwa sababu kwake, kusali kulikuwa tabia yake ya kawaida. Katika mazungumzo hayo ya moyoni, Yesu alimwita Mungu kama Baba na kuishi kwa uhusiano wa kina/ndani naye. Basi, tuko mbele ya uhusiano wa Mwana na Baba. Hakika wanafunzi wake walimwona akisali mara nyingi nao walitaka kujitambulisha na mwalimu wao hata katika shughuli hii. Hivyo mmojawapo alimwambia, “tufundishe!”
       Wakati Yesu alipowafundisha wanafunzi wake kusali, hakika aliwakabidhi maneno ambayo aliyatumia katika uhusiano wake na Baba na kuwakumbusha kuhusu mahitaji ya kuwa na tabia kamili, yaani tabia ya mwana anayemwomba Baba kwa imani. Hii ni tabia ya kujisalimisha mikononi mwa Huyo anayejua mahitaji ya wana kabla ya wamwombe kitu. Yesu hakuhitaji kusali kwa sababu ni Mungu aliye mmoja na Baba; hata hivyo, alisali sana. Kwa upande wake mtu anapaswa kusali sio tu anapohitaji bali kwa sababu hii ni sehemu muhimu ya safari yake ya kuishi, kama vile kula chakula, kunywa maji ama kupumua. Sehemu ya kwanza ya sala hii ni utambulisho wa ubaba wa Mungu, ambao unaonyeshwa kupitia utunzaji na wema wake. Huu ni mwaliko wa kulitukuza jina la Mungu, yaani, “Baba yetu… jina lako litukuzwe!” na mambo yote ambayo yanakuja baada ya maneno “Baba yetu…” yanayategemea maneno haya. Kulitukuza jina la Mungu ni kumpa Mungu utukufu wake kufanya Mapenzi yake kama Yesu alivyo, hasa aliposema “Chakula changu ni kufanya mapenzi ya Baba yangu.” Ni lazima kufanya mapenzi ya Mungu ili Ufalme wake utokee duniani kama mbinguni.
        Tunapaswa kumwelekea Baba huyo kwa imani, sisi tulio na uhakika kwamba tumepokea sana. Tunaomba kwa ajili ya mkate, ya msamaha na ya upatanisho. Kulingana na Maandiko matakatifu, “kutokana na wema wake tumepokea neema juu ya neema”. Ushuhuda huu ni uthibitisho wa utunzaji wa upendo wa Mungu anayeshiriki zawadi zake na wana wake, kutarajia kwamba tufanye vivyo hivyo kwa ajili ya wengine ili undugu kati yetu uwe maonyesho ya ubaba wake na chombo cha huruma yake. Sala Baba Yetu yadhihirisha kwamba sisi tuna mahangaiko kuhusu hali ya wengine na sio kuhusu mahitaji yetu ya kibinafsi tu. Sala hii inatufundisha kuomba kwa ajili ya lililo muhimu sana, yaani, “mkate wa kila siku”. Kwa sababu gani? Kwa sababu tunapaswa kupigana dhidi ya aina yote ya ukusanyaji na ubadhirifu wa chakula ambao unauharibu undugu, kuwafanya maskini na wenye njaa wateseke. Kuhusu mambo haya Baba Mtakatifu Francisco asema: “Ulaji umetuongoza kutumia chepesi pamoja na ubadhirifu wa chakula cha kila siku... Tunapaswa kukumbuka kwamba chakula ambacho sisi hutupa takatakani ni kama ikiwa tulikuwa tumeiba kutoka meza ya walio maskini na wenye njaa.”

Kwa Mt. Yohana Calabria, sala “Baba Yetu ni Injili kwa ufupi. Matatizo yote yapaswa kufikiriwa na kusomeka kwa maelewano na ubaba wa Mungu.” Ikiwa tunasema “Baba Yetu” ni kwa sababu tunasadiki kwamba sisi ni ndugu wa wengine wengi. Mungu hawabagui watu na hamsahau yeyote wa wana wake. “Kikundi chochote cha kidini kinapoanza kufikiri na kutenda kama kwamba Mungu yuko nao tu na sio watu wengine huko ni kumbinafsisha Mungu.” Yeye hapendezwi na sala ambayo inawaacha ndugu wengine. Mungu hatupatii daima yale tunayomwomba, bali anatupatia daima tunayohitaji. Ikiwa hatupokei yale tunayomwomba yeye ni kwa sababu hatuombi ipasavyo. Pamoja na kutufundisha kusali Yesu anatufundisha kuishi. Tunaalikwa kuishi kwa undugu kutokana na uzoefu wa ubaba wa Mungu na kuwa na tabia kamili katika ushusiano wetu naye, yaani kuwa na tabia ya wana, kwa sababu mtu ambaye haishi kama mwana hapati kutenda kama ndugu. Roho Mtakatifu aliye zawadi kubwa ambaye Baba alitupa kwa sababu ya wema wake, atusaidia kusali kama Yesu alivyofundisha, yaani, kwa njia kamili. 

Fr Ndega
Mapitio na marekebisho: Serah

Nenhum comentário: