domingo, 14 de agosto de 2016

HATARI YA KUMILIKI MALI NI KUMILIKIWA NA MALI


Kutafakari kuhusu Mhu 1,2;2,21-23; Kol 3,1-5.9-11; Lk 12,13-21

Masomo ya siku ya leo ni mwaliko wa kwelekea kwa uangalifu katika mambo ya mbinguni kwa sababu tumefufuliwa pamoja na Kristo na tumerithi zawadi za kimungu kupitia yeye. Maisha yetu yanaonja hali mpya ambayo yanafikiria mambo yaliyo juu kuwa muhimu zaidi kuliko mambo ya dunia. Ili tuweze kuendelea na safari yetu kwa maana, tunapaswa kumtegemea Mungu katika mambo yote.
Kuhusu injili tunataka kutafakari kuhusu mambo muhimu mawili, yaani maana ya maisha yetu na maana kamili ya mali katika maisha yetu. Kuhusu maana la maisha yetu, Yesu alisema kwamba “Uzima wa mtu haumo katika wingi wa vitu alivyo navyo.” Yesu anafikiria kwamba Maisha yanathamini zaidi kuliko mali. Tukumbuke yale aliyomwambia kijana tajiri, yaani “Nenda na kuuza ulicho nacho, ukawapa maskini na kunifuata”. Mali ilipotumika kwa ajili ya upatanisho na ndugu ni chombo cha wokovu; tukumbuke mkutano wa Yesu na Zakayo: “Leo wokovu umeingia katika nyumba hii, alisema Yesu.”
Wakati wa Yesu kilianza kipindi kipya ambapo wasiwasi na mahangaiko ya kawaida katika maisha yalikuwa  hayana maana tena. Yesu aliweka wazi kuwa mshikamano na familia haipaswi kumzuia mtu kumfuata. Mfano, mtu fulani alisema: “Nipe ruhusu ili niende kumzika baba yangu.” Yesu alimwambia, uache wafu wazike wafu wao...” Wakati ambapo wafuasi walikuwa bado hawajagundua upya wa ufalme wa Mungu, mali ilionekana kuwa usalama wa maisha ya baadaye. Sasa Yesu analeta mtazamo mpya. Lengo la uwepo wake miongoni mwa wanadamu ni kuwasaidia kugundua tena nafasi maalum ya Mungu katika maisha na ahadi kwa ajili ya jirani. Mali haiwezi kuchukua nafasi ya Mungu katika maisha yetu wala kutuzuia kuwasaidia wengine. Kwa hivyo Yeye (Yesu) anatuuliza swali, yaani, “Vitu ulivyojiwekea tayari vitakuwa vya nani?” kutokuwa na jibu kuhusu swali hili kunaonyesha kwamba tuko mbali sana na matarajio ya Yesu ambaye aliweka lililo njema kwa ajili ya wengine kama kipimo cha kuishi vizuri, yaani, kwa maana.
Zawadi tumepokea kutokana na ukarimu wa Mungu, hatuwezi kutumia kwa njia ya kibinafsi peke yake. Njia ya mafanikio ya maisha yetu sio kuwa na kitu bali kushiriki kitu. Anaposhiriki zawadi zake nasi Mungu anatufanya vyombo vya ukarimu wake kwa sababu anatarajia kwamba tuweze kutenda kama yeye alivyo. Tunatambua kwamba umo ndani yetu mwelekeo wa kumiliki na kuongeza mali, na kama matokeo, kadiri tunavyokuwa na mali, tena kadiri tunavyokosa kwa unyeti mbele ya hali ya walio na mahitaji mengi. Basi, ingawa mali inaweza kuwa msaada kwetu, injili hii inatukumbusha kuhusu hatari ya kuwa na wingi wa vitu ambavyo ninatufanya kuwa kama vipofu mbele ya hali ya wengine. Wakati tunaposhiriki kile tulicho nacho kwa ajili ya wengine “tutajitajirisha kwa Mungu.”  
Yesu anatuonya kwamba kutafuta usalama na furaha katika mali ni ndoto ya uongo kwa sababu mbili: ya kwanza, kadiri tunavyokuwa na mali, ni kadiri hiyo hiyo tunavyozidi kuwa na tamaa ya kupata zaidi; ya pili, tunapotafuta mali, hatutosheki wala kutulia. Basi, hatari ya kumiliki mali ni kumilikiwa na mali na kusahau hali ya kimungu na ahadi kwa ajili ya ndugu. Hatuwezi kusahau kwamba Mungu alituumba kwa ajili yake hatutulii mpaka tutakapotulia katika yeye (Agostino wa Hippo Afrika Kaskazini). Katika mali hatutulii, tutatulia katika Mungu.

Katika Matendo ya Mitume Luka anatoa picha ya jumuiya ambapo watu wanawashirikisha maskini mali zao, kiasi ambacho “hakuna mtu yeyote aliyetindikiwa kitu” (Mtd 4, 34).  patakuwa tena na yeyote atakayekosa mahitaji. Sisi ni wasafiri hapa duniani, na tutakapokufa hatutachukua chochote pamoja nasi (Sir 11:19). Mungu tu ndiye utajiri na tumaini letu la kudumu, na kitu kingine chochote ambacho hakituleti karibu na Mungu na wenzetu ni mbatili mtupu. Tukifikiria ufupi wa maisha tungempa Mungu nafasi ya kwanza katika maisha yetu. Tunaalikwa kutumia mali yetu kama kuendeleza kazi ya Mungu, kusaidia maskini, wateteaji amani. Hivyo tutatumia mali yetu kwa njia ya imani. Tunaweza kusema kwa kutumia maneno ya Zab 90:12, yaani, “Ee Mungu utufundishe ufupi wa maisha yetu ili tuweze kuwa na hekima.”

Fr Ndega 
Mapitio na marekebisho: Serah

Nenhum comentário: