sexta-feira, 20 de setembro de 2019

WASIMAMIZI WAMINIFU WA ZAWADI ZA MUNGU



Kutafakari kuhusu Am 8, 4-7; 1Tm 2, 1-8; Lk 16, 1-13



       Mungu anatarajia kwa watu wake maisha marefu na ya heshima. Mambo yote ambayo hayaisaidii hali hii yanakataliwa na Mungu. Hivyo, kupitia nabii Amos, katika somo la kwanza, yeye (Mungu) anashutumu aina yote ya ukandamizaji ambao uliwazuia watu waishi kama watu wa Mungu hasa hali ya udhalimu dhidi ya maskini na wenye njaa. Mateso yao yadhihirisha kwamba tuko na jamii ya kijeuri ambapo wako baadhi ya watu wenye nguvu ambao wanamiliki mali na pesa nyingi wakati wengine wengi hawana kilicho cha kutosha kwa kuishi.

      Kama dhambi ya kijamii ni matokeo ya kiasi cha dhambi za kibinafsi, hivyo, hata sisi tuko na jukumu katika hali hii ya udhalimu. Kuhusu hayo Baba Mtakatifu Francisco asema: “Ulaji umetuongoza kutumia vitu chepesi pamoja na ubadhirifu wa chakula cha kila siku... Tunapaswa kukumbuka kwamba chakula ambacho sisi hutupa takatakani ni kama ikiwa tulikuwa tumeiba kutoka meza ya walio maskini na wenye njaa.” Hali ya watu hawa ilikuwa kipaumbele katika kazi ya Yesu ambaye alichukua ahadi ya kuwa maskini ili kuwatajirisha wote kwa umaskini wake.    

     Katika somo la pili, Mt. Paulo anatushauri kuwaombea watu wote hasa wale ambao wako na mamlaka ya kuongoza na kutawala, yaani Viongozi wa Kanisa, Serikali na kadhalika. Hao wanapaswa kufanya kazi yao vizuri ili tuweze kuishi maisha ya utulivu na amani. Sisi ni wa Mungu na kwa hivyo, kazi ya viongozi wote kwa ajili ya maisha yetu ni ushiriki katika utawala wa Mungu mwenyewe ambaye hutaka watu wote waokolewe, na kupata kujua yaliyo kweli ama Aliye ukweli.  Ni jukumu letu ili watawale vizuri nalo linampendeza Mungu.

     Tukiendelea kutafakari kwetu, tuko na mfano ambao Yesu alisimulia kuongea kuhusu mahitaji ya kuwa mwaminifu kuhusu jukumu ambalo tumepokea kutoka kwa Mungu. Kile kilicho nacho kinatoka kwa Mungu kwa sababu vyote vizuri vyatoka kwake. Anatukabidhi utunzaji wa vyote na kutarajia tupate kusimamia zawadi zake kulingana na mapenzi yake. Sisi sio walio na mali bali ndio wasimamizi tu wa zawadi za Mungu. Hivyo, tunapaswa kuitumia pesa sio kama lengo la maisha, bali kama chombo cha kuizaa hali nzuri kwa wote.

     Tunaishi katika jamii ambapo pesa ni kipimo cha kila kitu na pia inaonekana kwamba pesa inatutawala. Kila kitu ambacho tunahitaji hakiwezekani kupata bila pesa. Hii ni nguvu na maana ya kuishi kwa watu wengi. Je, Wakristo wanapaswa kuwa na tabia gani mbele ya utajiri? Wale wanaofuata Kristo wanapaswa kuwa waaminifu katika mambo yote na kutumia tabia kamili kuihusu pesa. Kutokuwa na tabia kamili kuhusu jambo hili kunatuongoza kusahau haja ya uangalifu kwa ajili ya familia, utunzaji kwa afya yenyewe, uhusiano wa kweli na Mungu n.k.

      Mara nyingi uhusiano wetu na Mungu unasumbuliwa kwa sababu ya hamu ya kuwa na pesa na mali nyingi. Yesu hasemi kwamba pesa si muhimu, lakini asema kwamba haiwezi kutushika na kutumiliki. Yesu anataka tufahamu kwamba pesa haijengi thamani za kweli ambazo zinazaa uzima na furaha. Tunaweza kuitumia pesa ili kumtumikia Mungu, bali hatuwezi kumtumia Mungu ili tupate pesa. Tunapaswa kuwa macho kwa sababu hali hii inaweza kutokea na mara nyingi bila tutambue hiyo. Pesa ni kitu ambacho kinaweza kututumia na kutubadilisha kuwa wasio na hisia kwa ajili ya Mungu na kwa mahitaji ya wengine. 
    
      Pesa inatusaidia kuishi lakini imewaweka watu mbali sana wao kwa wao. Pesa inaijenga nyumba lakini inaweza kuharibu familia. Kupitia pesa tunaweza kuinunua nguo, chakula na kadhalika, lakini pia inaweza kuzaa upendeleo, ubaguzi na utoaji rushwa. Hatuwezi kuruhusu kwamba pesa iwe chombo cha tofauti kati yetu kwa kutuongoza kuwabagua wengine. Kati yetu tunajua jinsi vile pesa imekuwa muhimu, hasa kuhusu sadaka ya ukarimu kwa ajili ya kulijenga kanisa-hekalu na kwa ajili ya mahitaji mengi katika kazi zetu za kuinjilisha. Tunamshukuru Mungu kwa matumizi ya pesa kama maonyesho ya ukarimu kwa manufaa ya jumuiya zetu kwa kulijenga Kanisa la Bwana. Tena tumwombe neema ya kuwa na tabia kamili mbele ya pesa kwa kutumia ishara hii si kama chombo cha ubaguzi, bali kama chombo cha undugu.   

Fr Ndega

Nenhum comentário: