domingo, 20 de agosto de 2017

IMANI YA WENGINE NDIYO KUBWA


Kutafakari kuhusu Is 56, 1.6-7; Rom 11,13-15.29-32; Mt 15, 21-28


       Mungu anataka kuongoza njia ya mataifa kwa “nyumba” yake, yaani kwake mwenyewe. Yeye anawapenda wote na kutaka kuokoa wote. Yeye sio Mungu wa Israeli peke yake na hata Watu hawa walichaguliwa sio kwao wenyewe bali ili wawe chombo cha wokovu Mungu aliopanga kwa wote. Wokovu ni zawadi ya Mungu na hakuna mtu hata mmoja anayestahili zawadi hii. Mungu mwenyewe anawavutia watu kwake kwa sababu ya wema wake, lakini kipimo cha jibu kamili kwa mwaliko wake ni upendo na haki. Ndiye Mungu huyo ambaye Mt. Paulo anatangaza kama Mungu wa huruma kwa wote. Kupitia kazi hasa ya mtume huyo wale waliofikiriwa wa nge wa huruma hii wana nafasi ya kuionja vizuri. Ndio watu hawa ambao watawasaidia wale waliochaguliwa kwanza.

      Mathayo anasema kwamba Yesu alienda kukaa katika sehemu za Tiro na Sidoni. Zote hizi mbili ni wilaya ya Ugiriki, yaani ndiyo maeneo ya wasio Wayahudi. Yesu aliruhusu kuongozwa ili kukutana na watu wa nge wa Israeli. Mama mmoja alimjia Yeye na kupaza sauti: “Bwana, Mwana wa Daudi, nionee huruma! Binti yangu anasumbuliwa na pepo.” Mama huyo anaongea na Yesu kuhusu jambo la thamani kubwa mno maishani mwake, yaani, binti yake. Lakini mama huyo hapashi habari tu kuhusu binti yake, bali alimtambua Yesu kama Mwana wa Daudi na Bwana. Huyo mama Asiye Myahudi, hata anaweza kufundisha ‘watu’ wa Yesu mwenyewe jinsi ya kumkaribisha vizuri na kumwamini yeye. Basi, Yesu alifanya muujiza sio kwa sababu ya mahitaji ya mama huyo tu, bali hasa kwa sababu ya imani yake kubwa. Kama hitimisho tuko na ushindi wa imani.

      Majibu ya Yesu yalikuwa maneno magumu na mazito, yaani, “sikutumwa ila kwa watu wa Israeli waliopotea kama kondoo”; na jimbo lingine, yaani “si vizuri kuchukua  chakula cha watoto na kuwatupia mbwa.” Kweli ni ngumu kukubali na kufahamu kwamba maneno haya yatoke midomoni mwa Yesu kwa sababu tunajua kuhusu hisia zake mbele ya hali ya walio na mahitaji. Tunapaswa kufahamu kwamba andiko hili linatafsiri mtazamo wa Wayahudi kuhusu wokovu kama upendeleo wa baadhi ya watu. Hasa kati ya Wayahudi sio wote waliostahili kuokolewa. Yesu ndiye Myahudi lakini alitenda tofauti akikubali mwendo wa ‘kujifunza’ kuhusu lengo la kazi yake. Yeye aliruhusu kuongozwa na Roho kwenye Tiro na Sidoni na kila mkutano na watu ilikuwa nafasi ya kujifunza.

      Hasa kuhusu wanawake, Injili zote zinaongea juu ya uhusiano wa Yesu nao kama urafiki maalum. Hao waliandamana naye kutoka mwanzo mpaka mwisho wa maisha yake katika hali ya kibinadamu. Tukumbuke kwamba ndiye mwanamke mmoja (mamaye) aliyemwimarisha kuanza ufunuo wa Saa yake. Katika kifungu cha leo ndiye mwanamke mmoja (mgeni) aliyemwimarisha kuanza ufunuo wa utambulisho wake zaidi ya mipaka ya Israeli. Ndiye mwanamke mmoja (Magdalena) aliyekuwa wa kwanza wa kupokea habari ya maisha mapya ya ufufuko wake na jukumu la kuitangaza kwa wengine. Mtazamo wake na ishara zake za upendo kwenye wanawake zinawaimarisha kushinda hali ya dharau na ubaguzi katika jamii. Uhusiano wake nao unawahakikishia maisha mapya.


     Hali hii inadhihirisha kwamba Yesu sio mali ya Wayahudi. Kazi yake ni kwa wote kwa sababu alikuja kutimiza mapenzi ya Mungu anayetaka kuwaokoa watoto wake wote. Ingawa tunafikiria kwamba “tumeokolewa” na kufikiri kwamba maisha yetu yanampendeza Mungu, tunapaswa kuwa macho kwa sababu labda Mungu hana nafasi bado katika maamuzi yetu ya kila siku. Yesu anatufundisha njia ya kukutana na wengine na hata kushangazwa kuona imani yao kubwa. Kila wakati tunaalikwa kutambua kwamba imani haina mipaka na tena wakati tunakutana na wale wanao imani tofauti na yetu sisi tuko na nafasi ya kujifunza zaidi na kuimarishwa katika imani yetu. Mwendo huu unawezekana kwa sababu ni sehemu ya utambulisho wetu kama Wakristo kujifunza na kukua pamoja na wengine. Hatuwezi kusahau kwamba hata mwanamke wa injili ya leo anatufundisha sana hasa jinsi ya kuongea na Mungu. Kulingana na mfano wa mama huyo, ukubwa wa imani ya mtu unaonyeshwa na tabia ya uvumilivu na unyenyekevu kwa kuwaombea wengine kuliko yeye mwenyewe na kuwa na uhakika kuhusu msaada wa Mungu. Tunataka kumwomba imani hii. 

Fr Ndega

Nenhum comentário: