domingo, 11 de junho de 2017

MUNGU NDIYE USHIRIKA WA UPENDO


Mit 8: 22-31; Rum 5: 1-5; Yoh 16,12-15


        Tunaalikwa kutafakari kuhusu fumbo la Utatu Mtakatifu. Utatu Mtakatifu ni fumbo la Mungu aliye ushirika wa Baba na Mwana na Roho Mtakatifu. Yeye yu ushirika wa upendo kwa maana Mungu ni upendo. Upendo ni tabia ya Mungu. Hivyo, “Mungu ni Utatu kwa sababu ndiye upendo” (L. C. Susin). Mungu yu wa kipekee lakini haishi peke yake kwa sababu alitaka kuwa na kuishi kwa ushirika. Uumbaji wote ni uenezi wa nafsi na wa fumbo lake. Viumbe vyote vinaitwa kuingia katika mwendo huu wa upendo na kuwa maonyesho ya wema wake. Tumsifu Mungu kwa ushirika wake wa upendo, atukuzwe Baba na Mwana na Roho Mtakatifu... 

          Tunapofanya ishara ya msalaba, yaani, “Kwa jina la Baba na la Mwana na la Roho Mtakatifu”, tunaonyesha hisia yetu ya kuwa miliki ya Mungu na tena tunaongea kuhusu ukweli wa Mungu, ambaye yupo hapa na katika kila mahali. Yeye yu upendo aliye juu ya vyote na ndani ya vyote. Hivyo, anapatikana kwa wote lakini yeye ni fumbo daima kwa sababu hakuna lolote ambalo laweza kuweka mipaka kwako. Kulingana na Mtakatifu Agustino, “Mungu ni wa milele mno hata wakati yeye anapopatikana kuna yote ya kupatikana bado.” Kuna hadithi fulani ya Mtakatifu huyo ambayo inatusaidia kutafakari fumbo la Utatu Mtakatifu kama fumbo si la kufahamiwa bali la kukaribishwa. Ikiwa tunajifungua zaidi kwa fumbo hili tunaweza kuhisi zaidi tendo lake ndani yetu.

        “Siku moja Mtakatifu Agustino, aliye mchungaji na mwalimu wa kanisa, alikuwa akitembea katika pwani ya bahari, akijiuliza swali kuhusu fumbo la Utatu Mtakatifu, akisema, “inawezekanaje Mungu kuwako kama Mmoja na Utatu wakati huo huo?” Ghafla, alimwona mtoto mdogo aliyefanya shimo katika mchanga na kukimbia kwenye bahari, akachukua maji kidogo na kuyaweka shimoni. Baada ya kuangalia mchezo huu wa mtoto mdogo kwa mara nyingi, Agustino aliamua kumwuliza maana ya mchezo huo. Mtoto mdogo akamjibu akisema: “Najaribu kuweka maji yale yote ndani ya shimo hii”. Ameshangaa sana, Agustino akasema: “Hutapata kufanya hivyo kamwe!” Kisha, mtoto mdogo akamwambia akisema: “ni rahisi kwangu kuyaweka maji yale yote shimoni kuliko wewe upate kufahamu fumbo la Utatu Mtakatifu kwa akili yako. Mwishowe, mtoto mdogo alitoweka na Mtakatifu Agustino akajiambia: “Labda mtoto huyo angeweza kuwa ni malaika!”

          Ujumbe wa masomo ya siku ya leo unatusaidia kujifungua kwa fumbo hili, yaani fumbo la Mungu ambaye anajifunua kama Bwana wa historia na pia kama Mungu wa huruma kabisa. Ndivyo hivyo anaonyesha upendo wake. Kwa upendo huu anatoa Mwana wake kwa ajili ya kuokoa ulimwengu. Basi, wokovu wa ulimwengu ndio tendo la Utatu Mtakatifu, yaani Mwana alitumwa na Baba na kutenda kwa nguvu ya Roho Mtakatifu. Vile vile, Roho Mtakatifu alitoka kwa Baba kutuongoza kuelewa kamili mafundisho ya Mwana. Tunasadiki kwamba, kwa njia ya ubatizo, tumekuwa hekalu hai la Mungu na makao ya Utatu Mtakatifu. Roho Mtakatifu anaweka mioyoni mwetu pendo la Mungu akitufanya kuwa ni watoto wake na ndugu wa Yesu na kati yetu. Kwa kifupi, kwa njia ya Roho Mtakatifu tunaweza kumwita Mungu kama Baba yetu kwa uhuru kabisa.    


         Ujumbe wa uhusiano wa Utatu Mtakatifu ni msaada mkubwa ambao Ukristu unatoa kwa jamii yetu ambayo inaongozwa kwa njia ya ubinafsi na mashindano. Yesu alitukabidhi ujumbe wa upendo kama maana ya mambo yote. Tunaweza kuonyesha ukweli wa ujumbe huu ikiwa tunaishi kuungana naye (na  Utatu). Siku moja alisema “wote wawe na umoja; kama wewe Baba, ulivyo ndani yangu, nami ndani yako; hao nao wawe ndani yetu ili ulimwengu upate kusadiki.” Tunapoishi kwa uhusiano wa ndani na Yesu vivyo hivyo tunahisi ndani yetu tendo la Baba na Roho wake. Uzoefu wetu wa Yesu katika Ekaristi ni tena uzoefu wa Utatu Mtakatifu. Kulingana na fumbo hili, Mungu anatumikia, yeye yupo kati yetu na tena ndani yetu. Ndiye yeye mwenyewe anayetuunganisha naye na miongoni mwetu. Anafanya hivyo kwa sababu anataka tuwe washiriki katika uhai wake mwenyewe. Kwa hivyo, tuombe “Atukuzwe Baba na Mwana na Roho Mt... 

Fr Ndega
Mapitio ya Kiswahili: Christine Githui 

Nenhum comentário: