domingo, 3 de julho de 2016

UTAYARI KWA MAMBO YOTE KWA AJILI YA UFALME WA MUNGU


Kutafakari kuhusu Lk 10: 1-12, 17-20


          Yesu alikuwa na wanafunzi wengi. Alichagua kumi na wawili kati yao ili wawe mitume, lakini alipowatuma wamtangulie katika kila mahali, aliwatuma wote, hata wasio na cheo cha mitume. Jambo hili muhimu tunakuta katika toleo la Luka peke yake. Injili zingine, yaani, Marko na Mathayo, zinataja utume wa Thenashara peke yake. Kama namba Sabini na mbili ilikuwa namba ya mataifa yaliyojulikana katika mazingira yale, hii inamaanisha kwamba mataifa yote yanaalikwa kuikaribisha na kuishuhudia habari njema ya injili na uwepo wa ufalme wa Mungu. Ushuhuda wa wanafunzi utatokea kati ya nguvu ambazo zinaupinga mpango wa Mungu unaowaletea wote maisha mapya. Basi, kutangaza ufalme wa Mungu na kuwaponya wagonjwa ni kiini cha utume wa wafuasi wa Yesu. Ili waweze kupata mafanikio katika kazi, walipaswa kumtegemea Mungu katika mambo yote kama sehemu muhimu sana kati ya mwongozo waliopewa na Yesu ulio karibu sawa na ule wa mitume Thenashara. Waliporudi kutoka kazi walimpasha Yesu habari kuhusu mafanikio yao naye Yesu aliwahakikishia kwamba maana ya mafanikio hayo hayatoki kwao, bali yatoka kwa Mungu kwa sababu utumishi wao ni ushiriki tu katika kazi zilizo za Mungu mwenyewe.

        Msingi wa namba sabini na mbili tunaweza kukuta katika vitabu viwili vya Agano la Kale, yaani, cha Hesabu na cha Kutoka. Katika kitabu cha Kutoka namba 70 inatajwa tu miongoni mwa walioalikwa kwenda milimani Sinai pamoja na Musa. Katika kitabu cha Hesabu tuko na kuwekwa kwa wazee sabini wakati Musa alipolalamika kuhusu mzigo wa kuwatunza watu wote, akisema: “Siwezi kuwatunza watu wote hawa peke yangu; hilo ni jukumu kubwa mno kwangu!... Basi, Mwenyezi-Mungu akamwambia Mose, “wakusanyeni wazee sabini wa Israel, ambao wewe unajua wanaheshimiwa na kukubaliwa na watu kuwa viongozi... Nitashuka sehemu ya roho niliyokupa, niwape watu hao. Nao watabeba jukumu la kuwatunza watu hawa pamoja nawe (Hes 11, 14.16-117).” Pamoja na hao wazee wengine wawili ambao walikuwa wamebaki kambini walipokea pia roho na kutabiri bila kuacha (Hes 11, 26). Andiko hili linahitimika kuonyesha matarajio ya Musa kuhusu wito wa Watu wa Mungu wawe manabii. Kama andiko hili, Maandiko Matakatifu yote yanayashuhudia mahangaiko ya Mungu kuhusu maisha ya Watu wake na furaha yake ya kuwashirikisha wanadamu katika kazi ya wokovu wao wenyewe.

       Utume wa wanafunzi hawa unafanana na utume wa Yohane Mbatizaji, yaani walipaswa kutangaza ukaribu wa ufalme wa Mungu wakimtangulia Yesu ambaye alikuwapo na kutenda mema, lakini watu hawakumjua bado. Yesu akawatuma wawili wawili kwa sababu utume wa kuutangaza Ufalme wa Mungu si kazi ya mtu achukue peke yake. Ni kazi ya jumuiya nzima nayo ni lazima ichukuliwe pamoja. Yesu alisema kwamba ni muhimu kusali kwa sababu sala ni msingi wa utume na siri ya mafanikio yake. Aliushiriki uwezo wake nao pamoja na unyeti wake kuhusu hali ya mateso ya watu ili waweze kuwatumikia. Utumishi kwa watu ambao ni wa Mungu ni utumishi kwa Mungu. Kwa hivyo ni lazima kuwa macho kuepuka kuyatumia mamlaka hayo kwa njia mbaya. Ni jukumu lao kutangaza maisha kamili ya ufalme wa Mungu, lakini ikiwa watu hawalikubali pendekezo lao si jukumu lao tena. Wanafunzi wa Yesu wanapaswa kutenda kama mwalimu wao alivyo, yaani wanapaswa kuuheshimu uhuru wa watu. Habari ya ufalme inatokana na ukarimu wa Mungu nayo ni njema kwa sababu ni matokeo ya huria/hiari. 


      Sisi ni wanafunzi wapya wa Yesu na siku ya leo yeye anatarajia utayari sawa kutoka kwetu. Kwanza kabisa, tunapaswa kuwa macho kwa msukumo wa Mungu na kuzifuata nyayo za Yesu, kuchukua njia yake ya maisha, yaani njia ya unyenyekevu, na kufikiri tofauti na mwelekeo wa jamii. Kulingana naye mafanikio ya utume wetu yanawezekana ikiwa uzoefu wa kutenda pamoja unapata kushinda uzoefu wa kutenda kwa njia ya ubinafsi, kusaidiana katika jumuiya na kwa wema wa jumuiya. Tunapochukua kazi pamoja tunasaidiwa na wengine; hivi ni rahisi kufikia mafanikio yanayotarajiwa. Tunaweza kutangaza halisi ukaribu wa ufalme kupitia utumishi wetu wa ukarimu na wa hiari, kuheshimu wale wanaotenda tofauti nasi. Baadhi ya ugumu katika safari yetu tunapaswa kukabiliana kupitia roho ya sala na kujirekebisha daima. Ukarimu wetu katika safari ya wito uwe alama ya utayari wetu kwa mambo yote kwa ajili ya ufalme wa Mungu.   

Fr Ndega
Mapitio na marekebisho: Sarah

Nenhum comentário: