sábado, 3 de setembro de 2022

MASHARTI YA KUWA MWANAFUNZI WA KWELI WA KRISTO

    

Kutafakari kuhusu Lk 14: 25-33




 

    Umati wa watu waliandamana na Yesu, lakini sio wote waliokubaliana naye. Alipoitambua hali ya kutokuwa na ahadi na makubaliano, aligeuka na kuwaelekeza baadhi ya maneno. Maneno yake yalikuwa nafasi ya kutafakari kwa kweli maana ya safari yao. Ingawa Yesu alikuwa maarufu, kwa sababu ya mambo mema aliyofanya kwa ajili ya watu, utume ambao Yesu alichagua kutimiza mapenzi ya Mungu hauleti umaarufu. Watu waliamini kwamba Yesu alikuwa mpinduzi lakini hawajafahamu aina ya mapinduzi Yeye aliyoleta ulimwenguni. Walitaka kumfuata kwa njia yoyote.

    Kama Yesu hakuwa na nia ya kumdanganya yeyote, aliongea nao kwa uwazi sana kuhusu maana ya kumfuata na matokeo ya uamuzi huu. Njia hii ya kusema ilikuwa tabia yake ya kawaida kama alivyofanya kwa ajili ya wale kumi na wawili, yaani aliwajulisha masharti ili wawe wanafunzi wake wa kweli. Kutoka kwao, Yesu hakutarajia werevu ama upumbavu, bali upatikanaji, urafiki na imara. Hawawezi kumfuata Yesu kwa sababu walipokea habari tu ya kuwa ni vizuri kufanya hivyo. Yesu anatarajia zaidi, yaani mabadiliko ya ndani na kukubali mapendekezo yake kweli.

    Andiko hili ni mwaliko wa kuchukua ahadi ya kumfuata Kristo kwa kupanga mambo ya kesho, yaani kuwa na uwezo wa kuona mbele ili kuepuka kufaragua na udanganyifu. Ni vizuri kuota ndoto lakini ndoto hii inapaswa kuihusu hali halisi mtu anayoishi, vinginevyo itakuwa udanganyifu tu. Yesu anataka kuepuka kwamba safari ya wafuasi wake iwe pasipo maana ama ya udanganyifu. Ni lazima utambuzi, hekima, kupanga na uamuzi.

    Mungu mwenyewe anatupa mfano wa kuwa na mipango ya muda mrefu ili tupate mafanikio katika mambo yote tunayofanya kama wafuasi wa Yesu. Yeye Mungu alipanga kumtuma mkombozi ili kuokoa ulimwengu, kulingana na yaliyoandikwa: “... wakati maalum ulipotimia, Mungu alimtuma Mwanawe aliyezaliwa na mwanamke... ili apate kuwakomboa waliokuwa chini ya sheria.” (Wagalatia 4: 4-5). “Hata baadhi ya wakulima hutegemea mvua inyeshe hata kama hawajaandaa shamba mahali pa kupanda mbegu kama za mahindi au maharagwe.” Kupanga mambo ya kesho ni muhimu.

    Yesu alisema, “Basi, kadhalika kila mmoja wenu asiyeacha vyote alivyo navyo, hawezi kuwa mwanafunzi wangu.” Kama ilivyotekea katika vifungu vingine, Yesu aliwapendekezea watu mpango wa maisha unaojumuisha kujinyima, kwa sababu yeyote anayekutana na Yesu kwa kweli amekwisha pata hazina ya kweli kwa maisha yake wala hawezi kubaki alivyo, yaani mambo mengine hayana maana tena kama kwanza. Kwa maneno mengine, Yesu anataka kuwa kipaumbele maishani mwa wanaoamua kumfuata. Hakuna jambo lingine ambalo liweze kuitoa maana ya kweli kwa maisha yao ila Yesu peke yake.

    Wanafunzi wa Yesu wa kweli walimtegemea Mungu katika mambo yote kama Yesu alivyo. Yeye alishiriki na wanafunzi wake ufalme wa mbinguni na kuwajulisha njia ya msalaba ili waweze kufanya mapenzi ya Baba yake. Kupitia njia hii, tunatambua kwamba Kumfuata Yesu hakuuleti upendeleo au hadhi, bali mateso na kujisalimisha kwa ajili ya ufalme wa Mungu. Basi, yeyote anayetaka kuishi bila ahadi hawezi kumfuata Yesu. Tena yeyote ambaye anatamani kumfuata Kristo bila msalaba hatapata kumfuata kwa kweli kamwe.

    Kupitia njia ya unyenyekevu na utupu Yesu alipata utukufu. Utambulisho wa wanafunzi wa mwalimu Yesu unapaswa kufuata njia sawasawa naye. Kwa upande wa Kristo msalaba ulikuwa sehemu muhimu katika mwendo wa kufanya mapenzi ya Mungu na kudhihirisha kwa mpango wa upendo wake. Kwa upande wetu kama wanafunzi, kuchukua msalaba ni ishara ya utayari wetu kwa mapenzi ya Mungu kwa kujitolea kama Kristo. Kwa kufikia lengo hili tunapaswa kujikana sisi wenyewe ili Mungu aweze kujifunua kwa nguvu yote ya upendo wake. Tunapaswa pia kujiondoka kutoka katikati, yaani mahali muhimu ili wengine waweze kuwa na nafasi ya kwanza. Kwa maneno mengine, tunapaswa kuwafikiria wengine ni wamuhimu kuliko sisi wenyewe. Kama haiwezekani kumfuata Kristo bila msalaba, mfano wake wa uaminifu kwa mpango wa Mungu utuimarishe katika safari yetu ya yetu ya kujitolea kwa ajili ya ufalme wa Mungu.


Fr Ndega

Nenhum comentário: