Mostrando postagens com marcador UFUFUKO. Mostrar todas as postagens
Mostrando postagens com marcador UFUFUKO. Mostrar todas as postagens

domingo, 16 de abril de 2017

UZOEFU UNAOZAA UZIMA UNAOSHINDA MAUTI


Kutafakari kuhusu At 10,34a.37-43; Col 3,1-4; Yoh 20,1-9


Tufurahi sote, kwa sababu hii ni siku aliyotufanyia Mungu! Tangazo la ufufuko wa Yesu ni mwaliko wa furaha, yaani furaha ya maisha ambayo yanayashinda mauti, furaha ya upendo ambao unaushinda uchungu na kutembea kama rafiki katika njia za watu wa Mungu akiyaimarisha matumaini yetu. Wanafunzi wa kwanza walipotangaza tukio hilo, walianza kutokana na maisha ya Yesu ya kibinadamu, aliyetiwa na Mungu kwa kazi ya wokovu wa binadamu. Kwao Wanafunzi wa kwanza uzoefu walioishi pamoja na Yesu ulikuwa umejaa maana. Kutokana na uzoefu huu waliweza kuwa mashahidi. Basi, tangazo lao halikuwa maneno peke yake bali uzoefu wa maisha pia, yaani maisha yao yalibadilika. Kama alama ya wema wa Mungu, maana ya maisha ya Yesu ilikuwa kuwatendea watu mema. Matendo yake yote mengi yaliwezekana tu kwa sababu Mungu alikuwa pamoja naye.
Ikiwa Kristo hakuwa amefufuka, je, mahubiri ya wanafunzi wake yangekuwa na maana gani? Hakika yangekuwa tupu, yaani, pasipo maana. Mbele ya kifo kisicho na haki cha mwalimu wao walikufa moyo sana, lakini ushindi wa uhai unawapa maana mpya ya kuishi. Basi, ujumbe wa wanafunzi unatafsiri pia ushindi dhidi ya hali ya hofu ambayo waliishi baada ya kifo cha Mwalimu, yaani kikundi chao kilivunjika. Kwa wanafunzi ilikuwa vigumu sana kuendelea kwa safari baada ya kukatishwa tamaa kwao kuhusu mwalimu Yesu ambaye walitarajia mengi, hasa awe mfalme mwenye nguvu. Lakini maisha yao yalibadilishwa kabisa baada ya kuona ushahidi wazi wa ufufuko wa Mwalimu, yaani kaburi tupu, vitambaa alivyolalia, na baadaye Yeye mwenyewe akajionyesha kwao; kisha waliacha hofu, wakiitoa nafasi kwa imani na kuchukua maisha ya mashahidi.     
Lakini tunapaswa kutambua kwamba safari hii ya imani ya wanaume iliimarishwa na ushuhuda wa mwanamke mmoja anayeitwa Maria Magdalena ambaye alikuwa wa kwanza kuenda kaburini akutane na Yesu na kupokea habari kwa ajili ya Mitume. Walialikwa kukaribisha njia mpya ya Yesu ya kuishi kati yao na kuyaamini Maandiko yasemayo kwamba alipaswa kufufuka kutoka wafu. “Magdalena ni yule ambaye Yesu aliponya kwa kufukuza mashetani saba ndani yake. Katika Biblia namba saba inamaanisha ukamilifu. Basi, Maria Magdalena alikuwa ameponywa na Yesu kikamilifu.” Katika uhusiano na Kristo Maria alikuta upendo wa kweli ambao alikuwa ameutafuta sana kwa muda mrefu. Mwanamke huyo alijifunza jinsi ya kuwa mwanafunzi wa kweli, akimfuata Yesu wakati wa mahubiri, tangu Galilaya hadi msalabani. Kwa hivyo anastahili cheo cha “Mtume wa Mitume wa Yesu.” 
Baada ya kupokea habari kuhusu udidimizi wa mwili wa Kristo, wanafunzi wawili wakaenda mbio kuelekea kwenye kaburi, yaani Petro na mwanafunzi aliyependwa na Yesu (Yohane). Walikimbia pamoja, lakini huyo mwanafunzi alifika kwanza. Kama hivi ni upendo ambao unapaswa kufika kwanza katika kila kitu. Yule anayependa anapata kuwa wa kwanza katika maonyesho ya upendo na imani. Anaweza kutambua mabadiliko kandokando yake, kwa sababu yeye mwenyewe ana moyo ambao umebadilishwa na uzoefu wa kujiona kupendwa. Anaweza kushuhudia kuwa bila uzoefu wa upendo wa kweli imani yetu ni haba na bila maana.

Uzoefu wa ufufuko ni uzoefu wa upendo wa hiari na mwaminifu wa Mungu ambaye anaendelea kufanya upya mambo yote na kutuchagua ili tuwe mashahidi wa hali hii mpya. Tena ni uzoefu wa imani ambayo inakuta msingi wake katika Maandiko Matakatifu yanayoshuhudia kwa Yesu Mfufuka. Huu ni pia uzoefu wa ahadi ambao unatuimarisha kama wafuasi sio wa Mungu aliye mfu bali Mungu aliye mzima.  Upendo wake unazaa uzima katika sisi pia na kutufanya tuushinde vikwazo, hofu na mashaka yote. Kama ilivyotokea kwa wafuasi wa kwanza, sisi pia tunajaribiwa kufa moyo katika safari yetu, lakini Mungu anatutumia daima yeyote ambaye kama Maria Magdalena anatuletea habari inayofanya tofauti katika maisha yetu na kuonyesha njia tofauti ya kufikiri na kuishi imani. Ushuhuda wetu kama mashahidi wa Bwana Mfufuka uwe kama ilivyotokea na wanafunzi wa kwanza, yaani umejaa furaha na shauku.

Fr Ndega

sábado, 26 de março de 2016

TUFURAHI KWA SABABU BWANA WETU AMEFUFUKA


Kutafakari Kuhusu Lk 24, 1-12

Ndugu na dada zangu, tufurahi kwa sababu Bwana Yesu amefufuka! Amefufuka ili akae pamoja nasi na kutufanya watu wapya. Kufufuka kwake Yesu ni tendo la ajabu la Mungu na maana ya kweli ya maisha yetu. Kupitia Kristo Mfufuka uumbaji wote unafanyika upya. Mwanga wake unayaangaza magiza ya maisha yetu na kuufungua upeo wa macho wa uzima wa milele. Sikukuu hii ya ufufuko wa Bwana wetu inatualika kuishi furaha kubwa, yaani, furaha ya maisha ambayo yanayashinda mauti, furaha ya upendo ambao unaushinda uchungu. Yesu ni uwepo hai miongoni mwa wanadamu, kufufua matumaini yao. Ni nafasi nzuri ya kufanya upya ahadi yetu ya wanafunzi na kushinda hofu ambayo inatuzuia kuwa mashahidi wa kweli.
Masomo ya Agano la Kale yanatuonyesha mambo makuu ya Mungu ulimwenguni na hasa katika safari ya watu wake. Kupitia matendo ya Uumbaji, Agano, Ukombozi na Maisha mapya yeye anajifunua kuwa Mungu wa uhai na kutaka daima furaha kubwa kwa kila mmoja wa viumbe vyake. Furaha hii inatokana na uhai wa Utatu Mtakatifu, aliye ushirika wa upendo. Tangu uumbaji ametushirikisha katika uhai wake mwenyewe. Basi, uumbaji ulikuwa mwaliko wa tushiriki katika ushirika wa uhai na upendo wa Mungu. Matendo yake katika Agano la Kale hayakuwa kitu kingine ila kuwandaa watu wake kwa kuzaliwa upya kupitia ufufuko wa Mwanawe pekee. Hali hii ni wazi sana kupitia ubatizo ulio uzoefu wa ufufuko kwa njia maalum, kutufanya kuumba tena na kuchukuliwa na Mungu kama watoto wake tulio warithi pamoja na Mwanawe. Kwa maneno mengine, tunakufa na Yesu, kuzika hali zee ya wenye dhambi na kufufuka tena naye kama watu wamefanyika wapya kabisa.  
Katika injili, wanawake, yaani Mariamu Magdalene, na Yoana, na Mariamu mamaye Yakobo na wanawake wengine walikuwa na upendeleo wa kuwa mashahidi wa kwanza wa ufufuko wa Bwana. Waliamuka mapema asubuhi, kwa sababu waliimarishwa na upendo wa kweli kwa Yesu; upendo huu unawaongoza kumtafuta. Kwa muda, uzoefu wa ufufuko kwao ulikuwa kaburi tupu na tangazo la malaika, lakini ishara mbili zilitosha ili waweze kuishi tena furaha ya uwepo wa Bwana wao. Yesu hakuwako kaburini kwa sababu huko ni mahali pa wafu; naye ndiye alifufuka na kuishi milele. Habari njema hii ya furaha kubwa inapaswa kutangazwa. Baada ya tukio lililoonekana kuwa ushinde, yaani, kifo chake, Yesu aliruhusu uwezo wa kuziona ishara za ushindi wake kwanza kwa wale ambao walikuwa waathirika wa ubaguzi katika jamii na, kwa hivyo, walijiona waliotenganishwa. Kwa kweli kupitia chaguo hilo Yesu alithibitisha pendekezo lake la muda mpya, mawazo mapya na uhusiano mpya kati ya watu. kwa kufanya kazi muhimu ya tangazo la ufufuko, wanawake walipaswa kushinda hofu na mawazo kutoka jamii kuhusu wao wenyewe. Walikuwa na uhakika kwamba Mtu aliyechagua aliwaandamana nao daima.  

Kama wanawake na wanafunzi wa kwanza wengine, tunaalikwa kufanya uzoefu wa Bwana Mfufuka. Uzoefu huu siku hizi unaidai imani zaidi kuliko kugusa. Neno lake na ushuhuda wa wale waliotutangulia unatusaidia kushinda hofu na kuchukua ahadi ya kuwa mashahidi pia. Kupitia msaada wa wengine na msukumo wa Mungu tunaweza kushinda hofu zetu zote na kukubali kwa shauku utume wa kutangaza habari njema ya ufufuko wa Yesu. Yeye yupo miongoni mwetu na ndani yetu ili atufanye vyombo vya huruma yake. Uzoefu wa wanawake unatusaidia kumtafuta Bwana Mfufuka kwa mioyo yetu yote na kuruhusu kuongozwa na mwanga wake ili uwepo wetu uwe ufanisi katika mahali popote tuendapo. Uzoefu wa kumtafuta Bwana unatuwezesha kushinda vikwazo njiani, kutufanya mashahidi wa upendo ambao unauzaa uhai. Bwana Mfufuka anaishi miongoni mwetu! Tunapaswa kuwa macho ili tumtambue katika hali nyingi zinazoyahusisha maisha yetu. Yeye atupatie ujasiri ili tuwe mashahidi wake wa kweli.

Fr Ndega
mapitio na marekebisho: Sara